Rais wa Marekani Donald Trump anasema nchi yake ipo katika mazungumzo na maafisa waandamizi wa Cuba na anadhani pande hizo mbili “zitafikia makubaliano.”
Trump aliwaambia wanahabari Februari mosi kwamba Cuba ni “taifa lililoshindwa” na nchi hiyo haina tena Venezuela “kuiunga mkono.” Kisha akasema Marekani inazungumza na “watu wa ngazi za juu” nchini Cuba “ili kuona kitakachojiri.”
Trump hajafichua aina ya makubaliano anayolenga. Lakini ripoti katika Jarida la Wall Street inasema anatafuta “mabadiliko ya kiutawala” nchini Cuba ifikapo mwishoni mwa mwaka huu.
Trump aliwaambia wanahabari kwamba anataka watu “waliotendewa vibaya na Cuba” na kukimbilia Marekani wasaidiwe na waweze kurudi nchini kwao.
Amekuwa akiongeza shinikizo dhidi ya Cuba. Januari 29, Trump alisema taifa hilo la kijamaa linaweka “tishio la ajabu” kwa usalama wa taifa la Marekani, na akasaini amri ya rais ya kutoza ushuru wa ziada kwa nchi zinazoipatia mafuta.
Kuna wasiwasi unaoongezeka kwamba uhaba wa nishati na masuala mengine nchini Cuba yanaweza kuzorotesha hali ya kibinadamu nchini humo.