
Mvutano umeongezeka tena nchini Sudan mwishini mwa wiki hii iliyopita. Wanamgambo wa Vikosi vya Msaada wa Haraka (RSF) walizidisha mashambulizi yao dhidi ya Kordofan Kaskazini. Walitumia tena ndege zisizo na rubani kushambulia miundombinu muhimu ya kiraia na ya lazima katika mji wa kimkakati wa El-Obeid, ulioko kwenye makutano ya njia zinazounganisha sehemu tofauti za Sudan. Wanamgambo hao pia walishambulia mji wa Dilling katika jimbo hilo.
Imechapishwa:
Dakika 1 Wakati wa kusoma
Matangazo ya kibiashara
RSF ililenga eneo la viwanda la El-Obeid, Chuo Kikuu cha Kordofan, kituo cha matibabu, na vituo vingine vya kiraia. Kulingana na mamlaka ya Sudan, shambulio hilo lililenga maeneo yenye watu wengi katika jiji hilo, na kusababisha majeruhi, ingawa hakuna maelezo zaidi yaliyotolewa. Mashambulizi hayo yalisababisha hofu miongoni mwa wakazi.
Jeshi linadai kuwa lilidungua ndege tisa zisizo na rubani zilizohusika katika shambulio hilo. Wanamgambo wa RSF hawajajibu.
Siku ya Jumapili, Machi 1, Wanamgambo wa RSF walizindua shambulio kubwa la kushtukiza katika mji wa Dilling, ulioko yapata kilomita 160 magharibi mwa El-Obeid. Kulingana na jeshi, shambulio hilo lilizuiwa.
Dilling ilizingirwa na vikosi vya Abdelaziz al-Hilu, kiongozi wa Harakati ya Ukombozi wa Watu wa Sudan-Kaskazini (SPLM-N), mshirika wa RSF. Uingiliaji kati wa jeshi mwezi mmoja uliopita uliwawezesha wakazi wa mji huo kuweza kupata chakula.
Mbali na Darfur, majimbo matatu ya Kordofan, pamoja na Blue Nile, yamekumbwa na mapigano ya mara kwa mara na yanayoongezeka kati ya makundi ya wanamgambo na wanajeshi kwa miezi kadhaa, na kusababisha kuzorota kwa hali ya kibinadamu na usalama, haswa katika majimbo haya yaliyoathiriwa na migogoro.
Mwezi uliopita, Volker Türk, Kamishna Mkuu wa Haki za Binadamu wa Umoja wa Mataifa, alilaani mashambulizi haya ya ndege zisizo na rubani, ambayo yanaua zaidi raia na kuzidisha ugumu wa juhudi za kibinadamu.