LINDI: SERIKALI za vijiji vya halmashauri ya Wilaya ya Mtama mkoani Lindi zimepatiwa misaada ya vifaa vya ujenzi wa miundombinu ya shule, zahanati na kituo cha polisi ambao umegharimu zaidi ya Sh milioni 54 kupitia Shamba la Miti la Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) lililopo Rondo.
Ofisa Mhifadhi Mwandamizi wa TFS wa Shamba la Miti Rondo, Zephania Mduma amesema wakati wa kuekelea kilele cha maadhimisho ya siku ya Misitu Duniani na siku ya upandaji Miti kitafia inayofanyika kila mwaka Machi 21, na kwa mwaka huu inafanyika mkoani Lindi.

Amesema TFS kupitia shamba la miti Rondo imeweza kutoa msaada kwa jamii inayowazunguka ambapo kwa mwaka huu wa fedha 2025/2026, imetoa vifaa vya ujenzi vyenye thamani ya Sh milioni 7.5 katika Shule ya Mnara na ujenzi wa ofisi ya kijiji cha Mnara .

“Uwepo wa shamba hili la miti Rondo kumeiwezesha jamii inayotuzunguka kupatiwa misaada ya aina mbalimbali inayogharimu zaidi ya milioni 54,” amesema Mduma.
Mbali na misaada hiyo pia kupitia shamba la miti hilo, TFS imetoa miche zaidi ya 50,000 na kugawiwa wananchi wa vijiji mbalimbali vya taarafa hiyo ili wapande katika mashamba yao.

Amesema lengo ni kuwawezesha mashamba hayo kuwapatia mahitaji ya misitu karibu na mazingira yao na pia kupunguza utengemezi katika misitu ya asili na hivyo kupunguza uharibifu wa misitu.
Naye Mwalimu wa Mkuu wa shule ya Mnara, Onesmo Samwel ameushukuru Wakala huo kupitia Shamba la Miti Rondo kwa kuwapatia madirisha ya vioo na kufungwa katika jengo la kufundishia somo la Tehama (Kompyuta) kwa wanafunzi.
“TFS imetusaidia katika kuwezesha kuwa na jengo la darasa janja na wanafunzi wanajifunza kwa vitendo naa wanatumia vifaa vya Tehama kwa uhalisia na uweledi kabisa,” amesema Onesmo.
Mwalimu mkuu huyo amesema uwepo kwa wakala huo, shule hiyo imeandelea kunufaika kwa kupatiwa msaasa mingine ikiwemo saruji mifuko 65 iliyowezesha ujenzi jengo la mradi wa mashine ya kusaga nafaka kufanya misaada iliyowafikia ni zaidi ya Sh milioni 9 .
Kwa upande wake, Mtendaji wa Kata ya Mnara, Tarafa ya Rondo, Flora Munga kwa niaba ya wananchi ameushukuru wakala kwa kuwajali kutoa masaada huo uliowezesha kujengwa kituo cha Polisi cha tarafa na kukamilika kwa asilimia kubwa kikisubiri kufunguliwa rasmi.
Munga ametaja eneo lingine wanalonufaika nao ni kugawiwa miche ya miti ambapo kwa sasa wananchi wamkuwa na mwamko mkubwa wa kuwa na mashamba ya miti kutokana na kupambua faida zake.