SERIKALI ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imezindua rasmi ripoti ya uchambuzi wa mifumo ya kidijitali ya utoaji huduma za biashara na udhibiti (CART.IS), ikiwa ni sehemu ya juhudi za kupunguza urasimu na gharama za kufanya biashara.

Uzinduzi huo umefanyika jijini Dodoma kupitia Wizara ya Viwanda na Biashara kwa kushirikiana na Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Tanzania (TANTRADE), Kituo cha Biashara cha Kimataifa (ITC) na Umoja wa Ulaya (EU), kupitia mpango wa MARKUP II.

Akizungumza katika hafla hiyo, Mkurugenzi wa Maendeleo ya Biashara Wizara ya Viwanda na Biashara, Sempeho Manongi amesema matumizi ya teknolojia ya kidijitali si chaguo tena bali ni hitaji muhimu katika ushindani wa biashara duniani.

Uchambuzi wa CART.IS umebaini kuwa licha ya kuwepo kwa mifumo kadhaa ya kidijitali, bado kuna changamoto ya mifumo hiyo kutofanya kazi kwa pamoja, hali inayosababisha ucheleweshaji wa huduma na kuongeza gharama kwa wafanyabiashara.

Naye Mkurugenzi Mkuu wa TANTRADE, Latifa Khamis amesema mfumo huo utasaidia kuunganisha mifumo ya taasisi mbalimbali, kupunguza urasimu na gharama za miamala, pamoja na kuboresha kasi na ubora wa huduma za biashara. SOMA: ‘Tumeimarisha mazingira ya biashara, uwekezaji kukuza viwanda’

Kwa upande wake, mwakilishi wa ITC, Augustin Baret, amesema ripoti hiyo inatoa mwongozo wa wazi wa kuimarisha uratibu wa taasisi, kuboresha ubadilishanaji wa taarifa na kurahisisha taratibu za biashara. Utafiti huo ulihusisha taasisi tisa za serikali, huduma 33 za biashara na mwingiliano 92 kati ya taasisi, hatua inayoweka msingi wa maboresho ya kina katika urahisishaji wa biashara.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *