Kwa muda mrefu kambi ya wakimbizi ya Makpandu imeonekana kuwa kimbilio, lakini sasa imegeuka kuwa eneo la mashaka, na hofu. Bekia Mahadi Ali, mama wa watoto wanane aliyekimbia vita nchini Sudan akitarajia kupata hifadhi, sasa amejikuta akiishi kwa wasiwasi mkubwa baada ya ghasia kuibuka upya katika eneo hili. Furaha ya kupata usalama imetoweka, ulinzi umepungua, Bekia anahofia maisha yake na ya familia yake.

Hakuna usalama kabisa hapa kambini na tunaogopa, nilikimbia na wanangu bila baba yao. Watoto hawa ni jukumu langu, tulikuja hapa kutafuta kimbilio lakini hawawezi kwenda shule, sina cha kufanya. Ninachoomba tuhamishwe kutoka kambi hii,”

Wakimbizi katika kambi ya Makpandu wanaripoti kuwa watu wenye silaha huingia ndani ya kambi mara kwa mara, wakifyatua risasi hovyo, kuwatishia watu, na kupora au kuchoma moto mali za raia. Omar Ibrahim, ni mkimbizi mwingine kutoka Sudan, anafunguka.

“Wakati mwingine tunawachukua wanawake na watoto wetu kwenda kulala vichakani kwa sababu hakuna uhakika wa usalama ndani ya kambi. Hatuwezi hata kwenda shambani kulima. Tunaiomba Serikali na Umoja wa Mataifa waingilie kati, tulikimbia risasi nchini Sudan, lakini tumekutana na risasi zilezile tena hapa.”

Kufuatia shambulio la hivi karibuni lililosababisha kifo cha mkimbizi mmoja wa Sudan, kikosi cha Ujumbe wa Umoja wa Mataifa cha kulinda amani nchini Sudan Kusini, UNMISS, kimefanya doria katika kambi hiyo ya Makpandu ili kutathmini hali ya usalama. Thomas Bazawi, ni Afisa wa Ulinzi, Mpito na Urejeshwaji wa UNMISS, anafafnua jukumu lao.

“Jukumu letu ni kusaidia kurejesha imani kwa kushirikiana na jamii, mamlaka za mitaa, vikosi vya usalama na wengineo. Tunafanya kazi na wadau wote kuimarisha usalama ili watu waweze kujiamini na kuendeleza maisha yao tena.”

Umoja wa Mataifa unasisitiza kuwa uwekezaji katika amani kupitia mpango wa Hatua kwa Ajili ya Kulinda Amani (A4P) ni muhimu kwa usalama wa wakimbizi wanaokimbia migogoro ya silaha.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *