Mamlaka ya Masoko ya Mitaji na Dhamana (CMSA) imeendesha Shindano kwa Washiriki kutoka vyuo vikuu na taasisi za elimu ya juu yaani the Capital Markets Universities and Other Higher Learning Institutions Challenge lenye lengo la kujenga uelewa wa masoko ya mitaji na uwekezaji.
Shindano hili limetumia Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA), ikiwa ni pamoja na mitandao ya kielektroniki yaani simu za mikononi na intaneti. Shindano limegawanyika katika sehemu kuu mbili, ambazo ni (shindano la maswali na majibu – Quiz Competition) na (Shindano la kuandika Insha – Essay Competition).
Kupitia shindano hili, katika mwaka 2025, CMSA imeweza kuwafikia washiriki 28,393 ikilinganishwa na wanafunzi 20,000 waliotarajiwa, na hivyo kuvuka lengo la ushiriki na kupata mafanikio kwa asilimia 142. Idadi hii imefanya jumla ya wanafunzi walioshiriki tangu kuanzishwa kwa shindano hili kufikia 116,871. Mafanikio haya yametokana na jitihada za CMSA katika kuhamasisha wanafunzi kushiriki katika shindano hili, pamoja na matumizi ya TEHAMA kwa njia ya simu za mkononi, tovuti, na barua pepe.
Ofisa Mtendaji Mkuu wa CMSA, CPA. Nicodemus Mkama akitoa hotuba wakati wa hafla ya kutoa zawadi kwa washindi wa shindano la masoko ya mitaji kwa wanafunzi wa elimu ya juu na mahafali ya wahatimu wa mafunzo ya washiriki katika masoko ya mitaji.
Katika jitihada za kuhakikisha washiriki wanatumia elimu ya nadharia kwa vitendo, Mamlaka imefanikiwa kuweka utaratibu wa kuwawezesha washiriki wa shindano hili kuwa wawekezaji halisi, ambapo washiriki watatumia theluthi moja (1/3) ya fedha walizotuzwa kuwekeza katika hisa za kampuni zilizoorodheshwa kwenye Soko la Hisa la Dar es Salaam au katika mifuko ya uwekezaji wa pamoja iliyoidhinishwa na CMSA.
Kwa mwaka 2024, washindi wa shindano hili waliwezeshwa na CMSA kuwekeza shilingi milioni 10 katika makundi mawili, na leo hii uwekezaji wao umeongezeka na kufikia shilingi milioni 125 kwa kundi la kwanza; na milioni 128 kwa kundi la pili, sawa na ongezeko la asilimia 1,150 na 1,180 mtawalia.
Serikali yapongeza ukuaji na ustawi wa Masoko ya Mitaji
Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), amepongeza maendeleo ya masoko ya mitaji nchini Tanzania, akibainisha kuwa jumla ya thamani ya uwekezaji katika masoko ya mitaji sasa imefikia Sh 63.1 trilioni. Waziri alisisitiza kwamba ukuaji huu ni matokeo ya moja kwa moja ya sera zinazowezesha uwekezaji, usimamizi thabiti, na jitihada za kimkakati kama programu ya elimu kwa umma inayotolewa na CMSA.
Mhe. Waziri aliongeza kuwa Serikali imejikita katika kuunda mazingira yanayowezesha uwekezaji, yanayoendana na malengo ya DIRA 2050, kwa lengo la kuimarisha masoko ya fedha na kuchochea ukuaji wa uchumi. Aidha, Mhe. Waziri alibainisha kwamba mafanikio haya yanaonyesha uwezo wa masoko ya mitaji kuwezesha upatikanaji wa rasilimali fedha za kugharamia miradi ya maendeleo, kupanua fursa za uwekezaji, na kukuza uchumi wa nchi yetu.
Serikali yapongeza wataalamu wa Masoko ya Mitaji wenye weledi na ujuzi kimataifa
Katika jitihada za kuongeza idadi ya wataalamu wa masoko ya mitaji wenye ujuzi na weledi kwa viwango vya kimataifa, CMSA inashirikiana na Taasisi ya Kimataifa ya Dhamana na Uwekezaji (Chartered Institute for Securities and Investment – CISI) ya nchini Uingereza, katika kuendesha mafunzo yanayotambulika kimataifa. Mafunzo haya yameongeza ujuzi na weledi kwa wahitimu unaowawezesha kukabiliana na kasi ya mabadiliko ya maendeleo ya sekta ya masoko ya mitaji na dhamana ulimwenguni.
Katika kutekeleza mkakati huo, CMSA kwa kushirikiana na CISI imeendesha mafunzo kwa watendaji wa masoko ya mitaji hapa nchini, ambapo Mafunzo haya yamefanikiwa kupata washiriki 128, ikilinganiswha na lengo la kupata washiriki 80, na hivyo kuvuka lengo la ushiriki kwa kupata mafanikio ya asilimia 160. Kati ya washiriki 128 wa mafunzo hayo, washiriki 95, sawa na asilimia 74.2 wamefaulu mitihani inayokidhi viwango vya kimataifa na wamefanikiwa kutunukiwa vyeti na Mhe. Waziri wa Fedha.
Washiriki 12 wa juu wa shindano la masoko ya mitaji kwa wanafunzi wa vyuo vikuu wakipokea zawadi ya mfano wa tiketi ya ndege kwenda Nigeria kuhudhuria mafunzo kwa vitendo, ikiwa ni moja ya zawadi za washindi wa shindano hilo.
mafunzo haya yamekuwa chachu yenye matokeo chanya kwa maendeleo na ustawi wa masoko ya mitaji hapa nchini. Chini ya usimamizi wa CMSA, wataalamu hawa wamewezesha kuanzishwa kwa bidhaa mpya na bunifu katika masoko ya mitaji Tanzania.
Bidhaa hizo ni pamoja na hatifungani za kijani yaani green bond, hatifungani za jamii yaani social bond, na hatifungani zenye kukidhi matakwa ya Shariah yaani Sukuk bonds. Matokeo hayo yameiweka Tanzania katika ramani ya masoko ya mitaji ulimwenguni yanayotoa bidhaa bunifu zinazovutia wawekezaji wa ndani na wa kimataifa, hivyo kuchochea ukuaji wa uchumi hapa nchini.
CMSA itaendelea kutekeleza mikakati ya kutoa elimu kwa umma na kuendesha mafunzo kwa wataalamu wa masoko ya mitaji wenye ujuzi na weledi kimataifa.