RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi,Dk. Hussein Ali Mwinyi, amesema Serikali inaendelea na mikakati mbalimbali ya kuhakikisha zao la mwani linaongezewa thamani ili kuwanufaisha wakulima wake.
Rais Dk. Mwinyi ameyasema hayo Ikulu Zanzibar wakati alipokutana na Mwenyekiti wa Kampuni ya TSC Purple Limited, Stefan Kraan, pamoja na ujumbe wake waliowasili Ikulu, Zanzibar. Katika mazungumzo hayo, Dk. Mwinyi alieleza kuwa lengo la Serikali ni kuongeza uzalishaji wa mwani, kuhakikisha upatikanaji wa masoko ya uhakika pamoja na bei nzuri kwa wakulima.
Kwa upande wake, Dk. Kraan amesema kampuni hiyo inaendelea na ufungaji wa mitambo katika kiwanda cha kusarifu mwani kilichopo Chamanangwe, ambapo kazi hiyo inatarajiwa kukamilika mwezi Juni 2026 na uzalishaji kuanza rasmi mwezi Septemba 2026.

Ameongeza kuwa uwekezaji huo utaleta mapinduzi makubwa katika sekta ya mwani Zanzibar, ikiwemo uzalishaji wa bidhaa mbalimbali kama mbolea, chakula cha mifugo na dawa. SOMA: Mikakati inahitajika kupata soko la mwani EA
Vilevile, Dk. Kraan alimueleza Rais Dk. Mwinyi kuwa kampuni hiyo inapanga kuandaa mkutano mkubwa wa wadau wa kilimo cha mwani utakaofanyika Tanzania kuanzia Juni 16 hadi 19, 2026, pamoja na kufanya ziara maalum katika maeneo ya uzalishaji wa mwani Zanzibar kwa lengo la kubaini fursa mpya za kuendeleza sekta hiyo.
