
Huu ni uchunguzi wa kipekee wa RFI kuhusu vita vya vinavyoendelea katika bara la Afrika kati ya Kyiv na Moscow nchini Libya. Uchunguzi huu unafanyika kwa siri na unazingatia maslahi ya kiuchumi na kijeshi, pamoja na mapambano ya madaraka, ya Urusi na Ukraine, nchi mbili zilizoko vitani kwa zaidi ya miaka minne. Sehemu ya Pili: Je, afisa mkuu wa ujasusi wa Urusi aliuawa pwani ya Libya?
Imechapishwa:
Dakika 2 Wakati wa kusoma
Matangazo ya kibiashara
Kufuatia sehemu ya kwanza ya uchunguzi wa RFI, ambayo ilifichua uwepo wa vikosi vya Ukraine magharibi mwa Libya, kwa makubaliano na serikali ya Dbeibah huko Tripoli, tunaendelea kufichua mambo mengine ya mzozo kati ya Kyiv na Moscow barani Afrika, haswa nchini Libya.
Vikosi vya Ukraine vilishambulia meli mbili za Urusi zinazomilikiwa na sirika lisilo julikana. Afisa mkuu wa Urusi alikuwa ndani ya meli ya mafuta ya Urusi. Inaripotiwa kwamba aliuawa.
Kulingana na vyanzo vyetu vya Libya, takriban maafisa kumi wa ujasusi wa Urusi wa ngazi ya juu, waliojifanya mabaharia, walikuwa ndani ya meli ya mafuta ya Qendil. “Ni njia bora kwa maafisa wa ujasusi wa Urusi kusafiri,” moja ya vyanzo vyetu kimesema .
Shambulio hilo lilisababisha vifo vya watu wawili na saba kujeruhiwa. Jenerali Andrei Averianov, afisa wa ujasusi wa Urusi mwenye cheo cha juu zaidi, aliuawa, kulingana na vyanzo vyetu vya Libya.
Jenerali huyu alikuwa miongoni mwa waliopendekezwa kuchukua uongozi wa Wagner, ambacho sasa kinajulikana kama Africa Corps. Aliijua Afrika vizuri sana. Alifanya safari kadhaa nchini Libya. Hasa, alikwenda Benghazi, mashariki mwa Libya, ambapo alikutana na Marshal Khalifa Haftar.
Hili ni pigo kubwa kwa Urusi, ambapo taarifa hii haisambazwi. Moscow haijawahi kuthibitisha rasmi kifo hiki. Wala kukanusha.
“Kisasi cha Urusi?”
Moscow iliahidi majibu madhubuti kwa operesheni hii. Chini ya wiki moja baadaye, mnamo Desemba 23, Jenerali Mohammed al-Haddad, mkuu wa jeshi magharibi mwa Libya na afisa wa kijeshi wa cheo cha juu zaidi huko Tripoli, aliuawa nchini Uturuki. Ndege yake, iliyokodishwa kutoka kampuni binafsi yenye makao yake makuu Malta, ilianguka baada ya mlipuko ndani ya ndege, dakika chache baada ya kupaa kutoka Ankara. Aliambatana na mshauri wake Mohamed Diab, mkuu wa vikosi vya ardhini, Luteni Jenerali al-Fitouri Gribel, mkurugenzi wa huduma ya viwanda ya kijeshi, na Brigedia Jenerali Mahmoud al-Qatawi. Kwa jumla, watu saba wanaohusishwa na jeshi la Libya magharibi mwa Libya waliuawa.
Vyanzo vyetu vya Libya vinabaini kabisa kwamba hii ilikuwa jibu la Urusi kwa shambulio la Qendil. Hakuna tangazo rasmi lililotolewa tangu uchanganuzi wa visanduku viwili vyeusi. Hitimisho la uchunguzi ulioanzishwa kufuatia tukio hilo halijatangazwa na mwendesha mashtaka wa Libya. Ingawa baadhi nchini Libya wameishutumu Uturuki, wachambuzi wengine kadhaa na wanasiasa pia wanaamini kuwa ilikuwa kitendo cha “kisasi cha Urusi.”