
Polisi ya Sri Lanka imetangaza leo Alhamisi kukamatwa kwa wageni 231, hasa Wachina na Wavietnam, kufuatia uvamizi katika vituo vitatu vya ulaghai mtandaoni huko Colombo. Kukamatwa kwa watu hao kulifanyika katika operesheni tatu siku ya Jumatano na Jumapili, polisi imesema.
Imechapishwa:
Dakika 1 Wakati wa kusoma
Matangazo ya kibiashara
Washukiwa hao wamewekwa kizuizini hadi Mei 15 na uchunguzi wa kompyuta na simu za mkononi unaendelea.
Watuhumiwa “waliingia nchini kwa visa vya watalii na waliajiriwa kinyume cha sheria,” amesema msemaji wa polisi Frederick Wootler, akibainisha kuwa baadhi yao walikuwa wamepitisha muda wa visa zao.
Mnamo mwezi Machi, raia 135 wa China walikamatwa katika kesi kama hiyo kabla ya kufukuzwa nchini.
Wakati huo, ubalozi wa China nchini Sri Lanka ulisema kwamba ulishirikiana na mamlaka ili kuwazuia raia wake kufanya kazi katika vituo vya utapeli nchini Sri Lanka.
Kulingana na ubalozi huo, mtandao wa mawasiliano wa Sri Lanka ulioendelezwa vizuri, eneo lake la kijiografia, na urahisi wa kupata visa ulihimiza makundi ya matapeli mtandaoni kufanya kazi kutoka nchini humo.
Mnamo mwaka 2024, mamlaka ya Sri Lanka iliwakamata raia 230 wa China na Wahindi 200 kwa makosa kama hayo.