
Unguja. Wizara ya Utalii na Mambo ya Kale imekuja na vipaumbele 11 ikilenga kuimarisha vivutio vya utalii, kuvihifadhi na kuyaendeleza maeneo ya kihistoria Unguja na Pemba.
Ili kutekeleza vipaumbele hivyo, wizara imeomba Baraza la Wawakilishi kuidhinisha Sh65.627 bilioni.
Kati ya hizo Sh4.152 bilioni kwa kazi za kawaida, Sh3.948 bilioni kwa ajili ya mishahara na Sh57.525 bilioni kwa utekelezaji wa miradi ya maendeleo.
Akiwasilisha makadirio ya mapato na matumizi ya bajeti hiyo katika mkutano wa Baraza la Wawakilishi leo Mei 22, 2026, Kaimu waziri wa wizara hiyo, Mudrik Ramadhan Soraga amesema mipango hiyo inajikita kuongeza wingi wa wageni na kuongeza pato la Taifa.
Soraga amesema mpango mwingine wa wizara ni kuendeleza ushirikiano kati ya Wizara ya Utalii na Mambo ya Kale na Wizara ya Mambo ya Kale na Utalii ya Oman katika ukarabati na uendelezaji wa majengo ya kihistoria ya Mji Mkongwe.
Ametaja majengo hayo ni Makumbusho ya Amaan, Beit el Ajaib, Beit Oman, Beit Barghash, Sultan’s Palace, Grand Palace, Kasri la Mtoni na Kasri la Kibweni.
Kipaumbele kingine amesema ni utekelezaji wa ubia (PPP) katika ukarabati wa majengo ya kihistoria ya Mahakama Kuu ya Zamani ya Zanzibar, Ngome Kongwe, Mahamam ya Hamamni na Forodhani na Magofu ya Kihistoria ya Maruhubi, unaofanywa na Kampuni ya Infinity Cultural Development.
Hata hivyo, Soraga amesema wizara inakumbana na changamoto kadhaa ikiwamo ushiriki mdogo wa taasisi za Serikali katika kuitangaza Zanzibar kwenye masoko ya kimataifa na ushindani wa biashara ya utalii kutoka nchi zenye huduma na bidhaa zinazofanana na Zanzibar.
“Uvamizi wa biashara zinazotakiwa kufanywa na wazawa, badala yake kuchukuliwa na wageni kinyume na Sheria ya Utalii, pia matumizi haba ya mifumo ya kidijitali na AI katika kuitangaza, kuipima na kuiendeleza sekta ya utalii,” amesema.
Mjumbe wa kamati hiyo, Said Azana Hassan amesema kamati inaishauri wizara kuongeza kasi na bidii katika kuyahifadhi maeneo ya kihistoria ili kuzuia uvamizi huo.
“Kamati inahimiza kufuatwa kikamilifu kwa sheria ya utalii na kuhakikisha wageni hawakiuki sheria katika biashara hii ya utalii,” amesema.
Amesema kamati inaishauri Serikali kupitia Wizara ya Utalii na Mambo ya Kale kuendelea kuyafanyia matengenezo maeneo ya kihistoria ili kuleta haiba nzuri na ya kuvutia kwa wageni wanaotembelea maeneo hayo.
