
DAR ES SALAAM: Tanzania na Brazil zimekutana katika mkutano wa siku tatu kujadili namna ya kupambana na utumikishwaji wa watoto kwenye kilimo cha pamba kupitia mradi wa Cotton With Decent Work unaoratibiwa na International Labour Organization (ILO).
Mkutano huo umejikita katika kubadilishana uzoefu wa kukuza kazi zenye staha, usalama na afya kazini pamoja na hifadhi ya jamii kwa wakulima.

Mratibu wa Miradi Kitaifa wa ILO, Glory Blasio amesema changamoto za kiuchumi zimekuwa zikisababisha baadhi ya familia kuwapeleka watoto kufanya kazi mashambani badala ya kwenda shule. Amesema ushirikiano huo unalenga kuhakikisha watoto wanalindwa na wanapata haki zao za msingi.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Msaidizi wa Idara ya Kinga ya Jamii kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Ajira na Mahusiano Kazini, Frank Kilimba amesema wazazi wanapaswa kutumia mbinu za kisasa za kilimo badala ya kutegemea nguvu kazi ya watoto. Amesisitiza kuwa elimu ndiyo msingi wa maisha bora kwa mtoto.
