Dar es Salaam. Mshtakiwa Faki Shaal (54) na wenzake watatu wanaokabiliwa na mashtaka matatu likiwemo la kumiliki vipande 19 vya meno ya tembo yenye thamani ya Sh983 milioni, wataendelea kusota rumande kutokana na upelelezi wake kutokamilika.

Wakili wa Serikali Mwandamizi, Leonard Chalo ameieleza Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu leo Jumatatu Juni 1, 2026, wakati ilipotajwa.

Mbali na Shaal, washtakiwa wengine ni Khamis Hassan (40), Kenneth Twelve (54) na Mohamed Suleiman (43).

Wafanyabiashara hao wanakabiliwa na kesi ya uhujumu uchumi namba 10770/2026 yenye mashtaka matatu ambayo ni kuongoza genge, kujihusisha na nyaraka za Serikali na kumiliki meno ya tembo vyenye thamani ya Sh983 milioni, mali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

“Mheshimiwa hakimu, washtakiwa hawajaletwa leo mahakamani hapa, na upelelezi wake bado haujakamilika, hivyo tunaiomba Mahakama itupangie tarehe nyingine kwa ajili ya kutajwa,” amesema Wakili Chalo.

Chalo ameomba Mahakama itoe hati ya wito ya kuwapeleka mahakamani washtakiwa hao wakitokea rumande.

Ombi hilo lilikubaliwa na wakili wa utetezi, Abdurazack Kamwaga anayemtetea mshtakiwa wa pili (Hassan) na wakili Meshack Dede anayemtetea mshtakiwa wa nne (Suleiman).

Hakimu Ahmed baada ya kusikiliza hoja za pande zote mbili, alikubaliana na ombi la upande wa mashtaka na kutoa hati ya wito wa kuwapeleka washtakiwa mahakamani kutoka rumande, kwa sababu kesi hiyo leo imeahirishwa bila washtakiwa kuwepo.

“Nitatoa hati ya wito kwa washtakiwa hawa waletwe mahakamani tarehe ijayo, kwa sababu leo hawajaletwa na hapa mtandao inasumbua, tungeweza kuahirisha  kwa njia ya video, lakini tumeshindwa kutokana na mtandao kusumbua, hivyo tarehe ijayo washtakiwa waletwe,” amesema Hakimu Ahmed na kisha kuahirisha kesi hiyo hadi Juni 15, 2026 kwa kutajwa.

Kwa mara ya kwanza, washtakiwa hao walifikishwa mahakamani hapo Juni 10, 2026 na kusomewa kesi ya uhujumu uchumi.

Katika kesi ya msingi, washtakiwa wanadaiwa kati ya Machi na Mei 2026 katika Mkoa wa Mtwara na Dar es Salaam, kwa makusudi waliongoza genge la uhalifu kwa kukusanya, kumiliki na kupatikana na vipande 19 vya meno ya tembo vyenye thamani ya dola za Marekani 38,000 ambazo ni sawa na Sh983.23 milioni mali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Shtaka la pili ni kujihusisha na nyaraka za Serikali, tukio wanalodaiwa kulitenda Aprili 30, 2026 na Mei Mosi, 2026 jijini Dar es Salaam, walijihusisha kwa kusafirisha vipande 19 vya meno ya tembo vyenye thamani hiyo, bila kuwa na kibali cha Mkurugenzi wa Wanyamapori nchini

Pia, Mei 11, 2026 wakiwa eneo la Goba, wanadaiwa kumiliki vipande hivyo bila kuwa na kibali.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *