Dodoma. Hadi kufikia Aprili mwaka huu, Serikali ilishalipa deni la Serikali la   Sh9.74 trilioni ambalo ni asilimia 68.5 ya malengo yaliyotarajiwa kwa kipindi hicho.

Takwimu hizo zimetolewa leo Jumanne Juni 2,2026 na Waziri wa Fedha, Balozi Khamis Mussa Omar wakati akiwasilisha bajeti ya Wizara ya Fedha kw amwaka 2026/27.

Amesema katika kipindi cha kwa mwaka 2025/26, Wizara ilipanga kulipa kwa wakati deni la Serikali lililotarajiwa kuiva la Sh14.219 trilioni.

Amesema kati ya kiasi kilicholipwa, Sh4.5 trilioni zimetumika kulipa deni la nje wakati Sh5.3 trilioni zimelipa deni la ndani.

“Ufanisi katika ulipaji deni lililoiva, umeiwezesha nchi yetu kuendelea kuaminika katika masoko ya fedha ya kikanda na kimataifa, hapa nina furaha kulijulisha Bunge lako tukufu kuwa Tanzania imeibuka mshindi wa jumla katika Tuzo ya Usimamizi wa Deni la Umma katika nchi za Jumuiya ya Madola,” amesema Balozi Khamisi.

Amesema mbali na tuzo hiyo, lakini Tanzania imefanikiwa kupata tuzo  ya Ofisi Bora ya Usimamizi wa Deni la Serikali katika Kanda ya Afrika.

Katika hatua nyingine Balozi Khamisi amesema wameunda Sera ya Usimamizi wa Mali za Umma ambapo katika kipindi cha mwaka 2025/26, Wizara ilipanga kuandaa Sera ya Usimamizi wa mali za Umma kwa lengo la kuweka mwongozo wa kisera wa usimamizi na uratibu wa matumizi ya mali za umma.

Amefafanua hadi Aprili 2026, Wizara ilishakamilisha mchakato wa kukusanya taarifa kutoka kwa wadau, kufanya tathimini ya mahitaji na kuandaa rasimu ya awali ya Sera ya Usimamizi wa Mali za Umma na mikakati ya Utekelezaji na Mawasiliano itakayowasilishwa kwa wadau mara mchakato wa kuidhinisha Sera utakapoanza Julai 2026.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *