Dar es Salaam. Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalumu, Dk Dorothy Gwajima, ametoa wito kwa wanawake nchini kujijenga kiuchumi na kimaisha kabla ya kuingia katika mahusiano, akisema changamoto nyingi zinazoripotiwa katika ndoa na mahusiano zinatokana na kukosa maandalizi ya msingi ya maisha katika dunia ya sasa.

Kupitia ujumbe alioandika kwenye ukurasa wake wa Instagram, Gwajima amesema kuwa, kupitia uzoefu wake wa kupokea taarifa za migogoro ya mahusiano ya wanawake na wanaume, zaidi ya asilimia 90 ya malalamiko yanahusu wanawake wanaolalamika kutelekezwa na watoto, kukosa matumizi ya kifamilia na baadhi ya wanaume kushindwa kutimiza majukumu ya kifedha.

Amesema hali hiyo inapaswa kuwa funzo kwa wanawake na jamii kwa ujumla kujiuliza kama wanaingia katika mahusiano wakiwa wamejipanga au la, akisisitiza umuhimu wa elimu, ujuzi na kujitegemea kiuchumi.

“Binafsi huwa naanza kujiuliza, je, sisi walalamikaji huwa tunajiandaaje kwenda kukutana na yaliyomo kwenye ajenda tunayoikubali? Na kwa nini tuliacha shule, jamani? Hivi tunakuwa tulipatana na mpenzi kwa mapenzi au tulipatana na money downloading machine?” ameandika.

Gwajima ameongeza kuwa ni muhimu kwa wanawake kuacha dhana ya kutegemea kabisa wenza wao na badala yake wajenge msingi imara wa maisha yao kabla ya kuingia katika majukumu ya kifamilia ili kupunguza migogoro inayosababisha maumivu na malalamiko ya mara kwa mara.

Amesema baadhi ya changamoto zinazojitokeza katika ndoa zinachangiwa pia na watu kuacha elimu au kutojiandaa kimaisha, hali inayowafanya washindwe kukabiliana na changamoto za kiuchumi zinazojitokeza baada ya kuingia kwenye familia.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *