- Maiti aliletwa katika duka la jamaa mjini Nakuru kudai deni lake la shilingi laki nne alizokuwa amempa kuhifadhi
- Mwanamume huyo kwa jina Baba Martin hakuwa na budi ila kuangukia chaguo la miguu niponye
- Polisi wameshauri jamaa za mwendazake kuuzika mwili huo au kuurejesha katika hifadhi ya maiti
Kizaazaa kimeshuhudiwa katika kijiji cha Bondeni kaunti ya Nakuru baada ya jamaa za marehemu kuupeleka mwili wake kwa duka la jamaa anayesemekana kuwa na deni la marehemu.

Source: Facebook
Marehemu Richard Ogendi mwenye umri wa miaka 60 anasemekana kuhifadhi takriban shilingi laki nne kwa kundi linasimamiwa na jamaa huyo.
Mtuhumiwa anayefahamika kama Baba Martin alitoroka wakati wa kizaazaa hicho lakini jamaa za mwendazake wakaapa kuwa maiti hiyo haitaondolewa hapo hadi pale ambapo pesa hizo zitalipwa.
“Mjomba wangu alihifadhi kwa Baba Martin shilingi 400,000 kwa muda sasa. Tumemuita Baba Martin atueleze kwa kina kuhusiana na deni la mjomba wangu lakini amehepa,” alisema Benson Ongendi, mpwa wa marehemu.

Pia soma
George Ruto azua mjadala baada ya kudai aliwahi ‘kusota’ ile mbaya: “Nimekosa hata bundles”
Kwa mujibu wa wakaazi wa Bondeni, mtuhumiwa amekuwa na kesi kadhaa za kudaiwa japo tukio la Jumatatu – Februari 20 – ndilo litasalia katika kumbukumbu zao.
“Tumeona matukio mengi ya watu kuja hapa kumdai Baba Martin hela zao, wengine wanakuja hata na watu wa kumpiga. Watu wanamdai vitu kadhaa,” alisema Patrick Saad mzee wa kijiji.
Polisi hata hivyo wamewashauri jamaa za mwendazake kuupeleka mwili huo kwake Kisii kwa mazishi au kuurejesha makafani na kudai pesa hizo kupitia mahakama.
Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia news@tuko.co.ke au WhatsApp: 0732482690.
Chanzo: TUKO.co.ke