London. Serikali ya Uingereza imetangaza kuwa watoto wote wenye umri wa chini ya miaka 16 hawataruhusiwa kutumia mitandao ya kijamii kuanzia mwaka 2027, katika hatua inayolenga kuimarisha usalama wa watoto mtandaoni.

Akizungumza katika taarifa maalumu iliyorushwa moja kwa moja kwenye televisheni asubuhi ya leo Jumatatu, Juni 15, 2026, Waziri Mkuu wa Uingereza, Keir Starmer, amesema Serikali yake imefikia uamuzi huo baada ya kuongezeka kwa wasiwasi kuhusu athari za mitandao ya kijamii kwa afya ya akili, usalama na ustawi wa watoto.

“Marufuku kamili ndiyo uamuzi sahihi. Sipo tayari kufanya maelewano kuhusu usalama na furaha ya watoto wetu,” amesema Starmer.

Kwa mujibu wa Serikali, marufuku hiyo itahusisha majukwaa makubwa ya mitandao ya kijamii yakiwamo Snapchat, TikTok, YouTube, Instagram, Facebook na X.

Hata hivyo, programu za mawasiliano ya moja kwa moja kama WhatsApp na Signal hazitahusika katika hatua hiyo.

Wanasiasa wagawanyika

Tangazo hilo limeibua mjadala mpana ndani ya vyama vya siasa nchini humo, huku viongozi mbalimbali wakitoa maoni yanayokinzana kuhusu ufanisi wake.

Kiongozi wa Chama cha Conservative, Kemi Badenoch, ameunga mkono uamuzi huo na kusema ni hatua muhimu katika kuwasaidia wazazi kulinda utoto wa watoto wao.

“Ni habari njema kwamba Serikali hatimaye imeamka na kutambua hatari za mitandao ya kijamii kwa vijana,” ameandika kupitia mtandao wa X.

Hata hivyo, Badenoch ameishutumu Serikali ya Chama cha Labour kwa kile alichokiita “kubadili msimamo” baada ya awali kusita kuunga mkono marufuku hiyo.

Kwa upande wake, kiongozi wa Reform UK, Nigel Farage, amesema ingawa hatua hiyo inalenga jambo jema, itakuwa vigumu kutekelezeka kutokana na matumizi makubwa ya mitandao binafsi ya mtandao maarufu VPN.

Farage ameonya teknolojia hiyo inaweza kuwawezesha vijana kukwepa mifumo ya kuthibitisha umri wao kwa kuficha eneo walipo na utambulisho wao.

Aidha, ameeleza hofu yake utekelezaji wa marufuku hiyo unaweza kusababisha kuanzishwa kwa mfumo wa vitambulisho vya kidijitali kwa njia isiyo ya moja kwa moja.

Chama cha Liberal Democrats nacho kimeikosoa Serikali, kikisema hatua hiyo imeandaliwa kwa haraka bila kuweka mikakati madhubuti ya kuyawajibisha makampuni makubwa ya teknolojia.

Mapema mwaka huu, chama hicho kilipendekeza kuanzishwa kwa mfumo wa viwango vya umri unaofanana na ule wa filamu ili kudhibiti aina ya programu ambazo watoto wanaweza kutumia.

Kwa upande wake Chama cha Green kimesema ingawa kuna haja ya kuimarisha ulinzi dhidi ya madhara ya mtandaoni, marufuku ya jumla inaweza kuwa na athari zisizotarajiwa.

Chama hicho kimenukuu mashirika ya kutetea haki za watoto, yakiwemo NSPCC na Molly Rose Foundation, ambayo yameonya kuwa baadhi ya vijana, hususan wenye ulemavu wanaweza kujikuta wakitengwa zaidi na kukosa fursa za kupata msaada na ushauri kupitia mitandao ya kijamii.

Je, marufuku itafanikiwa?

Uingereza inafuata nyayo za Australia, ambayo Desemba 2025 ilitangaza marufuku kama hiyo na kuwa taifa la kwanza duniani kuchukua hatua hiyo.

Hata hivyo, ripoti za awali kutoka Australia zinaonyesha vijana wengi wameendelea kutumia mitandao ya kijamii kwa kutumia mbinu mbalimbali za kukwepa mifumo ya kudhibiti umri, hususan kupitia huduma za VPN.

Changamoto hiyo imeibua maswali kuhusu namna Serikali ya Uingereza itakavyotekeleza marufuku hiyo kwa ufanisi bila kuathiri haki za faragha za watumiaji.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *