
WATAALAMU wa maabara nchini wametakiwa kuzingatia kwa umakini mkubwa maadili na viapo vya taaluma yao ili kulinda jamii dhidi ya madhara yanayoweza kusababishwa na utunzaji usio salama wa vimelea hatarishi na smpuli zinazohifadhiwa kwa muda mrefu.
Wito huo umetolewa na Mratibu wa Afya Moja kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu), Valentino Sanga, wakati wa ufunguzi wa kikao kazi cha siku tano kinachofanyika jijini Arusha kwa lengo la kuimarisha usalama wa maabara na ulinzi wa afya ya jamii.
Sanga amesema mafunzo hayo yanatoa fursa kwa washiriki kubadilishana uzoefu, kujifunza miongozo ya kisasa na kukumbushana wajibu wao wa kitaaluma katika kuzuia na kubaini mapema vihatarishi vya kiafya. SOMA: Tanzania juu Afrika, huduma bora za maabara
Aidha, amesisitiza umuhimu wa kuhifadhi kwa usalama vimelea hatarishi na sampuli za maabara, akionya kuwa uzembe katika utunzaji wake unaweza kusababisha madhara makubwa kwa wataalamu na jamii kwa ujumla.
Jumla ya wataalamu 26 kutoka taasisi mbalimbali za Serikali na sekta ya afya wanashiriki katika mafunzo hayo yanayoungwa mkono na CIHEB-Tanzania kupitia Mradi wa Usalama wa Afya Duniani (GHS), kwa lengo la kuimarisha viwango vya usalama wa maabara nchini.