k

Chanzo cha picha, AFP

Iliyochapishwa

Muda wa kusoma: Dakika 4

Kwa karibu nusu karne, utabiri maarufu wa Pelé, bado unajirudia katika vichwa wa wachambuzi wa soka la Afrika, pale aliposema: Taifa la Afrika litashinda Kombe la Dunia kabla ya mwaka 2000.

Mwaka huo ulikuja na kuondoka, ukiacha tu mikosi kwa timu za Afrika. Kulikuwa na historia chache tu iliyoandikwa na Cameroon katika Kombe la Dunia 1990 kuwa nchi ya kwanza ya Afrika kufika robo fainali huko Italy.

Kisha Senegal ikafika robo fainali 2002 iliyofanyika katika nchi mbili za Japan na Korea Kusini. Na huzuni kubwa ikaipata Ghana ambao walikosa kwenda nusu fainali jijini Johannesburg, Afrika Kusini mwaka 2010. Kwa miongo kadhaa, hayo ndio mafanikio makubwa kwa Afrika.

Hadi pale Morocco ilipokuja kuvunja historia hiyo mwaka 2022 ilipofika nusu fainali kwa mara ya kwanza katika Kombe la Dunia lililochezwa Qatar.

Mambo yanabadilika

Timu za Afrika zina vipaji, ustadi, na uwezo, lakini kwa miaka mingi zimekuwa chini ya wababe wa Ulaya na Amerika Kusini. Lakini pengo hilo lililozoeleka kwa miaka mingi katika soka, sasa linapungua kwa kasi.

Droo ya 1:1 katika mechi ya kwanza kati ya Mabingwa mara tano wa Kombe la Dunia, Brazil na timu namba moja barani Afrika kwa mujibu wa Fifa, Morocco, imethibitisha hilo.

Chini ya kocha Walid Regragui, Morocco ilipata ushindi mbele ya Ubelgiji, Uhispania, na Ureno wakati wa mashindano ya Qatar. Ni miongoni mwa timu kubwa na bora za Ulaya.

Tofauti ya kihistoria kati ya mabingwa wa jadi wa kimataifa na soka ya Afrika haijapungua tu; inafutika polepole. Tunachoshuhudia kwenye timu za Afrika sio mkusanyiko tena wa wachezaji wa kawaida wanaofanya mambo ya hapa na pale yanayosababisha makosa.

Bali tunaishi katika enzi ya usawa wa kimuundo, kimbinu, na kisaikolojia. Timu kubwa hazijadhoofika; badala yake, Afrika imeboreka na kutikisa ubabe katika meza ya timu bora za mpira wa miguu.

Bila kujali matokeo, ya mechi ya Senegal na Ufaransa, au Senegal na England au Morocco na Uhispania au Morocco na Ureno; hizo hazihesabiwi tena kuwa mechi ndogo au mechi kati ya timu kubwa na ndogo.

Mvuto na presha ya mechi hizo barani Afrika ni kubwa kama vile Ureno ikicheza na Brazil au Uhispania dhidi ya England. Haya yote yanatoa jawabu kwamba kuna mabadiliko makubwa yanaendelea katika soka la Afrika.

Utandawazi wa Soka

K

Chanzo cha picha, Reuters

Mabadiliko haya ni matokeo ya moja kwa moja ya utandawazi wa akili za mpira wa miguu. Kizazi cha sasa cha nyota wa Afrika si wachezaji wanaogunduliwa wakiwa tayari washapitwa na umri; bali ni vipaji vinavyotengenezwa katika akademia bora za soka ulimwenguni.

Wakati wachezaji kama Achraf Hakimi, Mohamed Salah, na Victor Osimhen wanapotumia wikendi zao kucheza katika vilabu vikubwa vya mpira wa miguu barani Ulaya, hawapati tena shida ya udhalili wanapovaa jezi za timu zao za taifa.

Zaidi ya hayo, mazingira ya makocha wa ndani yamepitia mapinduzi. Enzi za ulazima wa makocha wa geni, umepitwa na wakati. Makocha waliokuwa wakisafiri kutoka Ulaya kuja Afrika miezi kadhaa kabla ya mashindano ili kulazimisha mfumo wa kigeni, kwa kiasi kikubwa mambo hayo yamekufa.

Timu za Afrika zinazidi kuongozwa na wataalamu waliokuzwa nyumbani ambao huchanganya elimu ya kimkakati ya soka, ya kiwango cha UEFA, huku wakiwa na uelewa wa kina na wa ndani wa kitamaduni na kisaikolojia za wachezaji wao.

Timu sita kati ya kumi zinazoshiriki Kombe la Dunia kwa sasa zinasimamiwa na makocha wazawa wa Afrika: Morocco, Ghana, Senegal, Ivory Coast, Tunisia na Cape Verde.

Nyuma ya kuziba pengo hilo kuna usawa wa sayansi ya michezo na uchanganuzi wa data. Kihistoria, timu kubwa za Ulaya zilikuwa na faida kubwa katika sayansi ya michezo, teknolojia ya matibabu, na utafutaji vipaji.

Leo, mafunzo ya mtoto katika Chuo cha Soka cha Mohammed VI huko Salé, Morocco, au chuo cha Génération Foot nchini Senegal yana vifaa sawa kama kizibao cha ufuatiliaji cha GPS, utaratibu wa lishe, na programu ya uchanganuzi wa video, kama mchezaji wa chuo cha Clairefontaine au Munich.

Bilashaka Afrika ina hamu ya mafanikio ya haraka na kuvunja rekodi ya Morocco, na kutimiza utabiri uliochelewa wa Pele. Hata ikiwa Afrika haikufanikiwa kubeba kombe mwaka huu, kwa hakika kasi ya maendeleo ya soka la ushindani wa timu za Afrika unatoa dalili kwamba lipo Kombe la Dunia ambalo litakuja katika bara hili.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *