
Waziri Mkuu wa Pakistani, Shehbaz Sharif amesema kuwa hafla ya kutia saini Mkataba wa Maelewano kati ya Iran na Marekani (MOU) itaandaliwa na nchi yake mjini Geneva, Juni 19 mwaka huu.
Sharif, ambaye nchi yake ilikuwa mpatanishi kati ya Iran na Marekani, alitangaza jana Jumatatu kwamba Tehran na Washington zimefikia makubaliano kufuatia mazungumzo ya kina, na pande zote mbili zimetangaza kusimamisha mara moja na daima operesheni zote za kijeshi katika nyanja zote, ikiwemo Lebanon.
Akizngumza jana katika hotuba yake ya ufunguzi katika Bunge la Taifa la Pakistani, Waziri Mkuu wa nchi hiyo Shehbaz Sharif alisema: “Leo, kwa neema ya Mwenyezi Mungu, ulimwengu umevuka hatua muhimu ya kihistoria.”
Akielezea mafanikio haya kama hatua ya mabadiliko baada ya kipindi cha mvutano wa kimataifa, Shehbaz Sharif amesema: “Nalipongeza taifa la Pakistani na jamii nzima ya kimataifa kutoka ndani ya moyo wangu.”
Ameyataja makubaliano kati ya Iran na Marekani kuwa suala la fahari ya pamoja, na kwamba Pakistan ilijitolea pakubwa kusaidia ushiriki huo wa kidiplomasia.
Jamhuri ya Kiislamu ya Iran na Marekani zilianza mazungumza ya kuhitimisha vita kikamilifu kwa upatanishi wa Pakistan baada ya kusitisha mapigano Aprili 8 mwaka huu.
Maandishi ya hati ya makubaliano (MOU) yaliyotokana na pendekezo la Iran lenye vipengee 14 tangu mwanzo wa usitishaji vita, yalikaguliwa mara kadhaa katika siku 60 zilizopita katika miji mikuu ya nchi zote mbili.