Imamu wa Msikiti wa Jumuiya ya Waislamu wa British Columbia (BCMA), Sheikh Ebrahim, ameshambuliwa katika tukio linalohusishwa na chuki dhidi ya Uislamu.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa Jumapili na Baraza la Kitaifa la Waislamu wa Kanada (NCCM), Sheikh Ebrahim alikuwa ameketi ndani ya gari lake baada ya kuongoza swala la jioni siku ya Alhamisi, ndipo mtu mmoja alipofungua kwa nguvu mlango wa gari lake na kumshambulia.

Taarifa hiyo ilieleza kuwa mshambuliaji huyo alikuwa akipaza sauti maneno ya chuki dhidi ya Uislamu na kumwambia: “Rudi katika nchi yako.”

Shirika hilo lilisema limekuwa likishirikiana na mamlaka katika saa 48 zilizopita ili kuhakikisha usalama na uwajibikaji kufuatia tukio hilo.

Taarifa hiyo iliongeza: “Kuona kiongozi wa dini anayeheshimika akilengwa na kushambuliwa kwa namna hii hakukubaliki kabisa.”

Pia ilionya: “Hili ni ukumbusho wa wazi wa hatari inayotokana na kuongezeka kwa chuki dhidi ya Uislamu inayoyakabili jamii zetu kila siku.”

Aidha, taarifa hiyo ilisema: “Hatuwezi kusimama kimya huku matukio kama haya yakiendelea kutokea kwa wingi wa kutisha,” na ikatoa wito kwa viongozi katika ngazi zote kulaani vurugu dhidi ya Waislamu na kuchukua hatua madhubuti kukabiliana na kuongezeka kwa chuki.

NCCM pia ilizitaka vyombo vya utekelezaji wa sheria kuchunguza vipengele vyote vya shambulio hilo, ikiwemo iwapo lilichochewa na chuki, na kuhakikisha kuwa mhusika anawajibishwa.

Katika ujumbe uliochapishwa kwenye mtandao wa kijamii X siku ya Jumapili, Waziri wa Utamaduni na Utambulisho wa Kanada, Marc Miller, alielezea shambulio hilo kuwa “la kusikitisha na la kinyama,” akisisitiza kuwa chuki dhidi ya Uislamu haina nafasi nchini Kanada.

Takwimu za Shirika la Takwimu la Kanada zinaonyesha kuwa ripoti za jumla za uhalifu wa chuki nchini humo zimekaribia kuongezeka mara tatu kati ya mwaka 2018 na 2025, hali iliyochangiwa kwa sehemu na ongezeko kubwa la chuki dhidi ya Uislamu pamoja na chuki dhidi ya Wayahudi.

Tangu utawala wa Israel uanze mashambulizi yake ya kimbari dhidi ya Gaza, yaliyosababisha kuuawa kwa karibu watu 73,000 na kujeruhi wengine 173,000, matukio ya chuki dhidi ya Uislamu nchini Kanada yameongezeka kwa takribani asilimia 1,800.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *