• Vita kali kati ya vyombo vya habari na wanasiasa vimechukua mkondo mpya baada ya K24 TV kuingilia mzozo unaoendelea kati ya Rais William Ruto na Standard Media Group
  • Kauli za kituo hicho zilichochea mabadilishano ya moto yaliyomhusisha Mbunge wa Kapseret, Oscar Sudi, rais wa zamani Uhuru Kenyatta na MediaMax
  • Wakati tuhuma, majibu ya tuhuma na barua za wazi zikisambazwa kwenye mitandao ya kijamii, mvutano huo umevutia umakini mkubwa huku siasa za kuelekea uchaguzi wa mwaka 2027 zikianza kushika kasi

Kilichoanza kama mgongano wa hadharani kati ya Rais William Ruto na Standard Media Group sasa kimeivuta K24 Television kwenye mzozo huo, na kusababisha vita vipya vya maneno vinavyowahusisha Oscar Sudi na rais wa zamani Uhuru Kenyatta.

Oscar Sudi anazozana na K24
Oscar Sudi alianzisha mashambulizi makali kwenye runinga ya K24, inayomilikiwa na kampuni ya habari inayohusishwa na aliyekuwa Rais Uhuru Kenyatta. Picha: Oscar Sudi, Uhuru Kenyatta.
Source: UGC

Mvutano huo mpya umeibuka baada ya Ruto kuikosoa hadharani Standard Media Group pamoja na mmiliki wake, aliyekuwa Seneta wa Baringo, Gideon Moi, akimtuhumu kutumia kampuni hiyo ya habari kuendesha kile alichokitaja kama kampeni endelevu ya propaganda dhidi ya serikali yake.

Pia soma

Ruto afichua kilichovunja maridhiano yake na Gideon Moi baada ya miezi minane ya usuhuba

Kauli za rais zilizua mjadala mkubwa huku Standard ikitetea nafasi yake kama chombo huru cha habari chenye jukumu la kuwawajibisha walio mamlakani.

Alhamisi, K24 Television, ambayo inamilikiwa na MediaMax inayohusishwa na rais wa zamani Uhuru Kenyatta, ilionekana kuingilia mjadala huo kupitia barua ya wazi iliyomwelekezwa kwa Ruto.

Katika ujumbe huo, kituo hicho kilikosoa mashambulizi ya Ruto dhidi ya vyombo vya habari na kuyahusisha na kumbukumbu ya vijana wa Kenya waliopoteza maisha yao wakati wa maandamano ya kupinga serikali.

“Mpendwa Rais William Ruto, wakati Kenya inaadhimisha miaka miwili tangu vifo vya vijana wa Gen Z waliokuwa waandamanaji, mashambulizi yako ya hadharani dhidi ya Standard Media Group yanatia wasiwasi mkubwa. Vyombo vya habari si adui yako. Uhuru wa vyombo vya habari si fadhila kutoka Ikulu. Ni haki inayolindwa na Katiba. Jukumu lake ni kuuliza maswali, kuripoti ukweli, kufichua mapungufu na kuwawajibisha walio mamlakani,” K24 ilisema.

Oscar Sudi amjibu K24 TV

Kauli hizo zilivutia haraka majibu kutoka kwa Oscar Sudi, mmoja wa washirika wa karibu na watetezi wakubwa wa Rais Ruto.

Pia soma

Hatua Kubwa ya Kidijitali: Wakenya Sasa Wapakua Vyeti vya Kuzaliwa Wakiwa Nyumbani

Katika chapisho lenye maneno makali, mbunge huyo alimshutumu Uhuru Kenyatta kwa unafiki na kudai kuwa MediaMax inatumika kuidhoofisha serikali ya sasa.

“Jayden (Uhuru Kenyatta), inaonekana una ugonjwa wa kusahau kwa kuchagua. Umesahau kwamba uliwahi kutuambia, ‘Gazeti ni ya kufunga nyama.’ Sasa unalazimisha kampuni yako mwenyewe, MediaMax, kuidhoofisha serikali ya sasa, jambo ambalo ni la kuchekesha. Naona umeungana na ndugu yako wa The Standard (Gideon Moi) katika kuanzisha mashambulizi. Karibu uwanjani!” aliandika Sudi.

Ruto with Gideon Moi at State House
A past image of President William Ruto with Gideon Moi at State House, Nairobi. Photo: William Ruto.
Source: Facebook

K24 yajibu Sudi kwa barua nyingine ya wazi

Dakika chache baadaye, K24 ilijibu kwa barua nyingine ya wazi, safari hii ikimlenga Sudi.

Kituo hicho kilisema kuwa kusahau kwa kuchagua katika uongozi hakuhusu tu kauli za zamani bali pia ahadi zilizotolewa kwa wananchi.

“Mpendwa Oscar Sudi, umemtuhumu Rais wa zamani Uhuru Kenyatta kwa kusahau kwa kuchagua. Hiyo ni kauli nzito, lakini pia inaleta swali kubwa zaidi: Kusahau kwa kuchagua kunamaanisha nini katika uongozi wa umma? Kusahau kwa kuchagua si tu kusahau kile mtu aliwahi kusema kuhusu magazeti,” K24 ilisema.

“Pia ni kuwasahau wapiga kura baada ya uchaguzi. Ni kusahau gharama ya maisha baada ya kampeni. Ni kuwasahau vijana wasio na ajira. Ni kuwasahau wazazi wanaohangaika kulipa ada za shule. Ni kuwasahau wafanyabiashara wadogo wanaokabiliwa na kodi kubwa,” kampuni hiyo ya habari iliongeza.

Pia soma

Magazeti ya Kenya Ijumaa, Juni 19: Wabunge 122 wapitisha Mswada wa Fedha 2026

Sudi alijibu tena, safari hii akielekeza ukosoaji wake moja kwa moja kwa utawala wa Uhuru na kumshutumu rais huyo wa zamani kwa kuiacha nchi ikiwa katika hali mbaya ya kiuchumi.

“Kusahau kwa kuchagua ni pale mtu anapoiacha nchi ikizama kwenye madeni makubwa huku akijua rais anayekuja atapata ugumu kuendesha uchumi. Kusahau kwa kuchagua ni pale mtu anaiba pesa zote za nchi na kuacha hazina ikiwa tupu huku akijua nchi itaanguka. Kusahau kwa kuchagua ni pale rais wa zamani Uhuru Kenyatta analewa na kusahau kuleta maendeleo. Aibu kwako, Jayden,” aliandika.

Read ENGLISH VERSION

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia news@tuko.co.ke au WhatsApp: 0732482690.

Chanzo: TUKO.co.ke

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *