
Morogoro. Jeshi la Polisi Mkoa wa Morogoro limetumia mkusanyiko wa mamia ya wafugaji kwenye sherehe za kimila za kimasai kutoa onyo dhidi ya uingizaji wa mifugo katika mashamba ya wakulima, likitaja tabia hiyo kuwa chanzo cha migogoro kati ya wakulima na wafugaji na kusababisha kutoweka kwa amani na utulivu.
Akizungumza na Mwananchi leo Juni 29, 2026 mjini Morogoro, Mkuu wa Polisi Jamii Mkoa wa Morogoro, Samweli Kijanga amesema ushiriki wao katika sherehe za kimila za jamii ya Kimasai zilizofanyika katika Kijiji cha Vianzi kilichopo Wilaya ya Mvomero, zimetoa nafasi kwa jeshi hilo kutoa elimu ya namna ya kujiepusha na migogoro ya ardhi.
Amesema Jeshi la Polisi linaendelea kutumia mikusanyiko ya kijamii kutoa elimu ya ulinzi, shirikishi na kuhimiza wananchi kuheshimu sheria pamoja na haki za wenzao ili kudumisha amani, na vitendo vinavyofanywa na baadhi ya wafugaji kuingiza mifugo katika mashamba ya wakulima kulazimisha migogoro isiyo ya lazima na isiyo na tija.
“Kila mfugaji ahakikishe mifugo yake hailishwi kwenye mashamba ya wakulima bila ridhaa ya wamiliki, kwa kuwa kufanya hivyo kunachochea migogoro ambayo inaweza kuepukika,” amesema Kijanga.
Mkazi wa Kijiji cha Vianzi, Mbaraka Ole Tangio amesema sherehe hizo za kimila huwahusu vijana wa kiume waliokamilisha tohara na kutambulika rasmi kama watu wazima wenye wajibu wa kushiriki katika shughuli za maendeleo ya jamii.
Ole Tangio amesema ujio wa Jeshi la Polisi katika sherehe hizo umeongeza thamani ya maadhimisho hayo kwa kuwapa wananchi elimu ya kudumisha amani na kuishi kwa kuheshimiana.
Kwa upande wake, mmoja wa vijana wa jamii hiyo, Paul Kasokwa amesema elimu iliyotolewa imewagusa vijana na wazee kwa pamoja na kuwa wataendelea kuhamasishana kuishi kwa amani na kushirikiana na wakulima kwa kuzingatia sheria na kaulimbiu yao ya “Tutatunzana”.