Timu nane pekee ndizo zimesalia kwenye mbio za kuwania taji la Kombe la Dunia, huku robo fainali zikitarajiwa kuanza Alhamisi hii nchini Marekani.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Dakika 4 Wakati wa kusoma
Matangazo ya kibiashara
Na Hannah Nalianya.
Mechi ya kwanza kuchezwa Alhamis kati ya Ufaransa dhidi ya Morocco
Ufaransa imeonesha ubora mkubwa na kupewa sifa zote kuwa miongoni mwa timu zinazopewa nafasi kubwa ya kutwaa ubingwa mwaka huu.
Ilimaliza hatua ya makundi kwa mafanikio, ikaiondoa Sweden, kisha ikaifunga Paraguay katika hatua ya 16 bora.
Ni vigumu kuona timu itakayoweza kuizuia safu ya ushambuliaji ya kocha Didier Deschamps, ambayo imejaa vipaji kama Kylian Mbappe, Ousmane Dembele, Bradley Barcola na Michael Olise.
Hata hivyo, Morocco ambayo haijapoteza mechi yoyote hadi sasa na haitatishwa na mabingwa hao wa dunia mara mbili.
Iliiondoa Uholanzi kwa mikwaju ya penalti kabla ya kuichapa wenyeji wenza Canada mabao 3-0 katika hatua ya 16 bora.
Atlas Lions wataingia uwanjani Boston wakiwa na nia ya kulipiza kisasi baada ya kufungwa na Ufaransa katika nusu fainali ya Kombe la Dunia la 2022 nchini Qatar.
Morocco iliweka historia mwaka huo kwa kuwa timu ya kwanza kutoka Afrika kufika nusu fainali na sasa inataka kurudia mafanikio hayo.
Uhispania dhidi ya Ubelgiji – Ijumaa Julai 10
Kwa kuifunga Ureno bao 1-0 Jumatatu, Uhispania imekuwa timu ya kwanza katika historia ya Kombe la Dunia kutoruhusu bao katika mechi sita mfululizo.
Kikosi cha kocha Luis de la Fuente, mabingwa wa Ulaya, huenda kisivutie kwa soka la muda wote, lakini ni chenye ufanisi mkubwa na kinamiliki mpira vizuri.
Nyota wa Barcelona Lamine Yamal amefunga bao moja pekee katika mechi tano, huku Mikel Oyarzabal akiwa amefunga mabao manne, yakiwemo mawili katika ushindi wa mabao 3-0 dhidi ya Austria katika hatua ya 32 bora.
Ubelgiji inaingia kwenye mchezo huo mjini Los Angeles baada ya kuichapa wenyeji wenza Marekani mabao 4-1, ambapo kabla ya hapo ilitoka nyuma kwa mabao mawili na kuifunga Senegal mabao 3-2 baada ya muda wa nyongeza katika hatua ya 32 bora.
Kombe hili la Dunia linaweza kuwa la mwisho kwa wachezaji waliosalia wa kile kinachoitwa kizazi cha dhahabu cha Ubelgiji, akiwemo Kevin De Bruyne na Romelu Lukaku, ambao watataka kumaliza safari yao kwa mafanikio.
Norway dhidi ya Uingereza – Julai 11
Mabeki wa Uingereza wamezoea kukabiliana na Erling Haaland katika Ligi Kuu, lakini swali ni kama wataweza kumzuia kwenye Kombe la Dunia.
Kikosi cha Thomas Tuchel kilifika Marekani kikiwa miongoni mwa timu zilizopewa nafasi kubwa ya kutwaa ubingwa kwa mara ya pili katika historia yake.
Nahodha Harry Kane na Jude Bellingham wamekuwa nyota wa Uingereza kwa muda sasa, wakifunga mabao 10 kati ya 11 ya timu hiyo, yakiwemo mabao yote matatu katika ushindi wa mabao 3-2 dhidi ya Mexico.
Uingereza ilibaki na wachezaji 10 lakini ikapambana hadi kuwaondoa wenyeji wenza, ushindi ambao umeongeza imani yao kabla ya mechi dhidi ya Norway.
Hata hivyo, watakutana na Norway mjini Miami, ikipewa nguvu na Haaland ambaye tayari amefunga mabao saba kwenye mashindano huku akiwania Kiatu cha Dhahabu.
Mshambuliaji huyo wa Manchester City pia amefunga katika kila moja ya mechi zake 14 zilizopita za mashindano akiwa na Norway, akifunga jumla ya mabao 27, na anatarajiwa kuipa changamoto safu ya ulinzi ya England.
Argentina dhidi ya Uswisi – Julai 12
Timu ya Argentina ya Lionel Messi imepitia nyakati ngumu kabla ya kutinga robo fainali dhidi ya Uswisi.
Mabingwa watetezi walilazimika kucheza muda wa nyongeza kabla ya kuiondoa Cape Verde, iliyokuwa ikicheza Kombe lake la Dunia kwa mara ya kwanza, kwa ushindi wa mabao 3-2.
Kisha katika hatua ya 16 bora walijikuta nyuma kwa mabao 2-0 dhidi ya Misri kabla ya kufanya mabadiliko makubwa ya mchezo, huku Messi akiwa kiungo muhimu wa ushindi huo.
Kocha Lionel Scaloni anafahamu kuwa timu yake haiwezi kuendelea kuitegemea bahati ikiwa inataka kutwaa taji la nne la Kombe la Dunia.
Hata hivyo, Argentina imeonyesha kuwa haiwezi kuhesabiwa nje ya mbio hizo.
Sasa watakutana na Uswisi mjini Kansas City.
Uswisi iliiondoa Colombia kwa mikwaju ya penalti mjini Vancouver baada ya sare ya bila mabao.
Uswisi pia imefika hatua ya robo fainali kwa mara ya kwanza tangu ilipoandaa Kombe la Dunia mwaka 1954, timu hiyo ina nidhamu kubwa na inatarajiwa kuwa ngumu kuivunja.