Dar es Salaam. Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kimeendelea kuwachukulia hatua viongozi wake waliojitokeza hadharani kumtuhumu Makamu Mwenyekiti wa chama hicho bara, John Heche, huku idadi ya waliochukuliwa hatua ikifikia watano.

Waliochukuliwa hatua ni Katibu wa Jimbo la Bumbuli, Abubakari Mashambo, aliyepokonywa wadhifa wake; Katibu wa Chadema Mkoa wa Morogoro, Barnabas Okola, aliyesimamishwa uongozi wake; pamoja na wenyeviti wa Chadema Wilaya za Mkinga na Kilindi mkoani Tanga, Amuli Shindo, Joseph Mwakidasi na Mathias Cosmas, ambao wamesimamishwa nyadhifa zao kuanzia leo Julai 11, 2026.

Mashambo na Okola wametakiwa kuwasilisha ushahidi wa tuhuma walizozitoa dhidi ya Heche ndani ya siku 14, kuwa amepokea michango ya fedha kutoka kwa wadau lakini huitumia kwa masilahi binafsi badala ya shughuli za chama.

Hatua hizo zilianza kwa Mashambo kuvuliwa wadhifa wake, ikafuatiwa na kusimamishwa kwa Okola, kabla ya uongozi wa Chadema Mkoa wa Tanga kutangaza jana Ijumaa kusimamishwa kwa Amuli Shindo na Mathias Cosmas kwa tuhuma za kukiuka kanuni za maadili ya viongozi wa chama.

Kwa mujibu wa taarifa iliyosainiwa na Mwenyekiti wa Chadema Mkoa wa Tanga, Jonathan Bahweje, viongozi hao wanadaiwa kutoa matamko kupitia vyombo vya habari dhidi ya makamu mwenyekiti wa chama bila kufuata taratibu za ndani, pamoja na kushindwa kuwasilisha hoja zao kupitia vyombo halali vya chama.

Bahweje amesema kusimamishwa kwao ni hatua ya muda kwa mujibu wa ibara ya 6.3.6(c) na (d) ya kanuni za chama, na kutadumu hadi mchakato wa kinidhamu utakapokamilika na uamuzi wa mwisho kutolewa kwa mujibu wa ibara ya 6.3.6(v).

Amesema katika kipindi hicho hawataruhusiwa kutekeleza majukumu yao ya uenyekiti wa wilaya wala kuzungumza au kutenda kwa niaba ya Chadema katika ngazi hizo.

Akizungumza na Mwananchi leo Jumamosi, Julai 11, 2026, Katibu wa Chadema Mkoa wa Tanga, Kaunya amesema hadi sasa viongozi wanne wamechukuliwa hatua, akiwemo Mwakidasi (Katibu Chadema wilaya ya Muheza) huku akidai chama kinafuatilia kwa umakini kile alichodai kuwa ni mpango unaoratibiwa wa kuwashawishi viongozi wake.

“Hii ni ‘project’ inayoratibiwa na watu fulani wanaowarubuni viongozi wetu kwa kuwapa fedha ili kuzungumza hadharani kuhusu Makamu Mwenyekiti,” amedai Kaunya.

Kauli hiyo iliendana na ile ya Katibu Mkuu wa Chadema, John Mnyika ambaye amesema chama kina taarifa za awali kuhusu watu wanaowashawishi baadhi ya viongozi kufanya mikutano ya waandishi wa habari na kutoa tuhuma dhidi ya Heche kwa malipo ya fedha.

“Mtu anapewa Sh2 milioni ili akazungumze hayo. Sasa ukishakuwa na madai hayo tuliyoyapata kabla, halafu matukio yakatokea katika hali ambayo kuna mpango unaendelea, hatua za kuchukua zinakuwa za tofauti sana,” amesema Mnyika.

Mnyika amesema katiba, kanuni na maadili ya Chadema yanamtaka kiongozi mwenye malalamiko dhidi ya mwenzake kuwasilisha taarifa kupitia vyombo vya ndani vya chama badala ya kuzungumza na vyombo vya habari.

“Kwenda kuzungumza na vyombo vya habari kuhusu madai yoyote, yawe ya ukweli au uongo, ni kinyume cha katiba, kanuni na maadili ya Chadema,” amesema.

Ameongeza kuwa viongozi waliochukuliwa hatua wana haki ya kukata rufaa iwapo hawajaridhika na maamuzi yaliyotolewa na uongozi wa kanda.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *