Dar es Salaam. Baba Mtakatifu, Leo XIV amemteua Padri Vincent Mpwaji wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam kuwa Askofu Msaidizi wa Jimbo Kuu la Dar es Salaam.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa leo Jumamosi, Julai 11, 2026 na Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC), uteuzi huo umefanywa na Baba Mtakatifu, huku Padri Mpwaji akitarajiwa kuanza majukumu yake ya kusaidia shughuli za kichungaji katika jimbo hilo.

Padri Vincent Lawrence Mpwaji alizaliwa Juni 5, 1978 mkoani Morogoro. Baada ya kuhitimu masomo ya upadri, alipata daraja takatifu la upadre Julai 7, 2008 jijini Dar es Salaam.

Katika kipindi cha utumishi wake, amehudumu katika nafasi mbalimbali ndani ya Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, akijipatia uzoefu katika shughuli za kichungaji na utawala wa Kanisa.

Aidha, ana Shahada ya Uzamivu katika Teolojia aliyoipata kutoka Chuo Kikuu cha Kipapa cha Gregorian kilichopo Roma, Italia.

Kabla ya uteuzi huo, Padri Mpwaji alikuwa akihudumu kama Chansela wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam na Paroko Msaidizi wa Kanisa Kuu la Mtakatifu Yosefu, Dar es Salaam.

Taarifa hiyo imesainiwa na Katibu Mkuu wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC), Padri Charles Kitima.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *