Dar es Salaam. Jeshi la Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, linamshikilia mkazi wa Mwananyamala, Hosamu Hamza maarufu ‘Maopena’, kwa tuhuma za kumuua baba yake mzazi pamoja na baba yake mdogo.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa leo, Jumamosi Julai 18, 2026, na Kaimu Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Faustine Mafwele, mtuhumiwa alikamatwa jana, Julai 17, saa 9 alasiri, katika eneo la Makongo akiwa na kisu kilichokuwa na madoa ya damu, huku mavazi aliyokuwa amevaa nayo yakiwa na alama za damu.

Taarifa hiyo imefafanua kuwa baada ya kukamatwa, mtuhumiwa huyo alipelekwa katika kituo cha polisi kwa ajili ya mahojiano na uchunguzi wa awali.

“Wakati mahojiano yakiendelea, jeshi la polisi lilipokea taarifa kutoka kwa wananchi kuhusu kutoweka kwa watu watatu waliokuwa wakiishi katika nyumba moja iliyopo Mtaa wa Sindano, Mwananyamala, huku damu zikionekana ndani ya nyumba hiyo,” imeeleza.

“Uchunguzi uliofanywa na wataalamu ulibaini miili ya watu wawili waliotajwa kuwa Hamza Juma Omari maarufu Mautila (48) na Ally Juma Omari (37),” ameeleza Mafwele.

Katika taarifa hiyo, Mafwele amesema uchunguzi wa kina wa awali ulibaini mtu anayedaiwa kufanya tukio hilo la mauaji na kuwafukia ni Maopena ambaye mtoto wa marehemu Omari ‘Mautila’.

Mafwele ameeleza kuwa sababu halisi za mtuhumiwa huyo kufanya tukio hilo la kuwaua baba yake mzazi na baba yake mdogo bado zinachunguzwa.

“Jeshi la Polisi linaendelea kuwashukuru wananchi na mamlaka zingine za kisheria na za kiuchunguzi wa kisayansi kwa ushirikiano wao na utoaji wa taarifa zenye mafanikio zinazoendelea kuwezesha uchunguzi wa tukio hili,” amesema Mafwele.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *