KLABU ya TRA United iko katika hatua za mwisho za kukamilisha usajili wa kiungo mshambuliaji, Franck Steve Belobo ambaye kwa msimu wa 2025-2026, kwenye Ligi Kuu ya Cameroon ya MTN Elite One ndiye aliyekuwa mchezaji bora wa msimu yaani (MVP).

Nyota huyo anayecheza nafasi ya kiungo mshambuliaji kwa ufasaha, aliibuka mchezaji bora wa msimu wa Ligi Kuu ya Cameroon ya MTN Elite One katika kikosi cha Canon Sportif de Yaounde, jambo lililoivutia TRA United kuiwinda saini yake haraka.

Usajili wa nyota huyo ni mapendekezo ya benchi la ufundi chini ya Kocha Mkuu, Mrundi Etienne Ndayiragije aliyehitaji kusajiliwa kiungo mshambuliaji wenye uwezo wa kutengeneza nafasi za kufunga na sasa dili hilo liko mbioni kukamilika.

Akizungumza na Mwanaspoti, Ofisa Habari wa TRA United, Christina Mwagala amesema timu hiyo imeingia kambini tangu Julai 15, 2026, kwa ajili ya maandalizi ya msimu mpya wa 2026-2027, japo suala la usajili bado linaendelea na halijakamilika.

Franck anaenda kuungana na wachezaji wengine wapya waliosajiliwa wakiwemo kiungo mkabaji, Mzamiru Yassin aliyejiunga na timu hiyo baada ya kuachana na Simba aliyoitumikia kwa miaka 10, tangu aliposajiliwa mwaka 2016, akitokea Mtibwa Sugar.

Mwanaspoti linatambua nyota wengine waliokuwa katika hatua za mwisho za kujiunga na TRA United katika dirisha hili la usajili ni viungo pia wakabaji, Salmin Hoza kutoka Dodoma Jiji na Greyson Gerald Gwalala kutokea timu ya Coastal Union.

Mbali na usajili wa nyota hao wanaoenda kuongeza nguvu katika kikosi hicho kwa ajili ya msimu ujao wa 2026-2027, ila pia timu hiyo inakaribia kupata saini ya beki wa kati wa Geita Gold, Charles Komanya baada ya dili hilo kufikia hatua nzuri.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *