GOLIKIPA Wilbol Maseke, amevunja mkataba na Coastal Union ya Tanga, baada ya kutofikia malengo yake na sasa anatafuta chalenji mpya kwa ajili ya msimu ujao huku akikiri anafanya mazungumzo na timu tofauti.

Wakati Maseke anajiunga Coastal, alisaini mkataba wa miaka miwili, uliyokuwa na kipengele cha akimaliza mmoja akipafomu asilimia 85 ataendelea na wa pili, lakini lilishindika hilo baada ya kipa huyo kucheza mechi chache.

Mwanaspoti lilimtafuta Maseke ili kujua anaenda wapi baada ya kuachana na  Coastal amesema :”Kuna timu za ndani na nje, ili bado sijaamua niende wapi na ndiyo maana siwezi kuzitaja, hivi karibuni nadhani kila kitu kitakuwa sawa.

Ameongeza:”Ingawa Coastal ilihitaji niendelee kusalia kikosini, mimi niliomba nikapate chalenji mpya, baada ya kuona msimu uliyoisha sikuwa na nafasi ya kucheza mechi nyingi, tumeachana kwa amani na nimefuata utaratibu unaotakiwa.”

Maseke ambaye kwa mujibu ya makaratasi amezaliwa Agosti  08, 2000 ( umri wa miaka 25), amesema bado ana ndoto ya kufanya vitu vikubwa kwenye mpira wa miguu, hivyo anahitaji nidhamu ya muda na kupambana zaidi.

“Mimi ni mtu ninayejitathimini nilikwama wapi msimu uliopita na kipi nikifanye kwa ajili ya msimu ujao hivyo bado nina nafasi ya kuonyesha makali,” amesema Maseke aliyewahi kuichezea Azam FC na KMC.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *