• Jaji wa Mahakama Kuu Cecilia Githua aliamua kuwa aliyekuwa gavana wa Migori Okoth Obado alikuwa na sababu kubwa ya kutaka kukatiza maisha ya Sharon Otieno
  • Jaji Githua alibaini kuwa Obado alikiri kuwa na uhusiano wa kimapenzi na Sharon Otieno uliosababisha ujauzito mwaka 2018
  • Katika hukumu yake, jaji alieleza kwa kina kile ambacho huenda kilimsukuma aliyekuwa gavana wa Migori kumuua Sharon

Nairobi – Jaji wa Mahakama Kuu Cecilia Githua Alhamisi, Julai 23, aliwahukumu aliyekuwa gavana wa Migori Okoth Obado na washitakiwa wengine wawili kwa mauaji ya Sharon Otieno, akihitimisha kesi iliyotikisa Kenya tangu kifo cha mwanafunzi huyo wa chuo kikuu mwaka 2018.

Okoth Obado
Jaji Cecilia Githua alimpata Okoth Obado na hatia ya kumuua Sharon Otieno. Picha: ODPP/Sharon Otieno.
Source: Facebook

Akitoa hukumu yake, Jaji Githua alieleza kwa kina kile ambacho huenda kilimsukuma aliyekuwa gavana huyo kukatiza maisha ya Sharon.

Sababu kuu iliyomfanya Okoth Obado kumuua Sharon Otieno ilikuwa ipi?

Jaji alisema Obado alikiri kuwa na uhusiano wa kimapenzi na Sharon Otieno, na kwamba ujauzito uliotokana na uhusiano huo ndio uliokuwa chanzo cha mlolongo wa matukio yaliyoishia kugharimu maisha ya Sharon.

Pia soma

Jamaa aangua kilio kortini baada ya Obado kupatikana na hatia ya kumuua Sharon

Jaji alieleza mwenendo wa Obado katika miezi iliyotangulia mauaji hayo. Alibaini kuwa mara kwa mara alimshinikiza Sharon kutoa ujauzito, na juhudi hizo ziliposhindikana, alisitisha msaada wa kifedha ambao alikuwa akimpatia hapo awali.

Kwa mujibu wa Jaji Githua, Obado aliwasiliana tena na Sharon baada ya kupata taarifa kwamba alikuwa amepanga kuweka wazi hadharani uhusiano wao, ikiwa ni pamoja na kuwafikia wanahabari. Mahakama ilibaini kuwa uwezekano wa suala hilo kuripotiwa na vyombo vya habari ulimpa sababu ya moja kwa moja ya kuchukua hatua dhidi yake.

“Kwa mtazamo wangu, mshtakiwa wa kwanza alikuwa na sababu kubwa sana ya kukatiza maisha ya Sharon kinyume cha sheria ili kuhakikisha kwamba uhusiano wao wa siri hauwekwi wazi kupitia vyombo vya habari vya kuchapisha,” alisema Jaji Githua.

“Hakuna shaka kwamba mshtakiwa wa kwanza ndiye ambaye angenufaika zaidi na mpango huo, kwa kuwa huenda angepata fedheha kubwa mbele ya umma kama marehemu angeweka wazi uhusiano wao.”

Sharon Otieno, mwanafunzi wa Chuo Kikuu cha Rongo, alitekwa nyara na kuuawa mnamo Septemba 2018. Mwili wake ulipatikana katika Msitu wa Kodera, Kaunti ya Homa Bay, ukiwa na majeraha mengi ya kuchomwa kwa kisu. Alikuwa na ujauzito wa miezi minane wakati alipouawa.

Pia soma

Okoth Obado na washitakiwa wengine 2 wapatikana na hatia ya mauaji ya Sharon Otieno

Kesi hiyo ilivutia hisia za taifa kutokana na nafasi ya juu ya Obado serikalini pamoja na ukatili uliotumika katika mauaji hayo. Obado, ambaye alikuwa gavana wakati huo, alikuwa miongoni mwa magavana wa kwanza waliokuwa madarakani nchini Kenya kushtakiwa kwa kosa la mauaji.

Uamuzi wa Jaji Githua ulieleza kuwa ushahidi uliowasilishwa ulimweka Obado katikati ya njama hiyo, huku mahakama ikiridhika pasipo shaka yoyote inayokubalika kisheria kuwa yeye na washitakiwa wenzake walihusika na kifo cha Sharon Otieno.

Read ENGLISH VERSION

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia news@tuko.co.ke au WhatsApp: 0732482690.

Chanzo: TUKO.co.ke

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *