Dar es Salaam. Waziri Mkuu Mwigulu Nchemba amemuagiza Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi) kukamilisha maandalizi mipakani kuelekea Fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) 2027.

Amesema mashindano hayo yanaandaliwa kwa ushirikiano baina ya Tanzania, Uganda na Kenya hivyo kutakuwa na muingiliano mipakani baina ya watu hivyo hakupaswi kuwa na changamoto yeyote.

Waziri Mkuu ametoa maagizo hayo leo Februari 23, 2026 wakati akizungumza na wananchi wa mji wa Namanga mkoani Arusha ikiwa ni sehemu ya ziara yake mkoani hapo.

“Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi na Tamisemi kaeni kukamilisha maandalizi kuhusu mambo ya mipakani kueleka AFCON.Mashindano haya tunaanda kwa pamoja na ni kweli huenda watu wakatoka huku na huku kwa ajili ya kufuata michezo itakapokuwa inachezwa Afrika Mashariki,” amesema

Mwigulu ameongeza kuwa, “tunajua sana wenzetu wa Kenya watapenda kuja kuangalia mpira wa Tanzania kwa sababu Tanzania kwa sasa ina mpira mkubwa kuliko yeyote hapa Afrika Mashariki.  Tumecheza 16 bora, kwa hiyo tuwe na maandalizi ya kuwawezesha watu wetu kupita huku na kule.”

Mbali na hayo, katika maagizo yake, Mwigulu amewaelekeza watumishi wote wa umma kuacha kuzoea matatizo ya watu kwani watu wanapofikisha changamoto zao kwenye ofisi za zao wanahitaji ufumbuzi.

Amesema sababu ya Serikali kugatua madaraka ni kuwezesha wananchi kutatuliwa kero zao kwa haraka ngazi za chini na zile ambazo haziwezekani kutatuliwa zielekezwe ngazi za juu.

Waziri Mkuu amesema habari ya kuwepo kwa watumishi wengi wa umma ambao wamejikita kujadili umbea na mambo binafsi ndani ya ofisi za umma haikubaliki.

“Hatutatumia lugha ya ustaarabu kwa wavivu, wezi na wazembe ndio. Tunataka wananchi wapate huduma, majawabu ya mambo yanayowasumbua katika ofisi zetu za umma,”amesema na kuongeza.

“Sisi viongozi tunakutana sana, wengine wakishamaliza kukaa kikao na kupokea maelezo wamemalizia hapo hakuna hata jambo lolote walilotoka nalo.”

Ushikiriano

Awali akimkaribisha Waziri Mkuu, Mkuu wa mkoa wa Arusha, Amos Makalla amesema upo ushirikiano mzuri kati ya Tanzania na Kenya kupitia mikutano ya ujirani mwema pamoja na mabonanza ya mpira.

“Hali ya mipaka yetu ya Kenya na Tanzania ni salama na biashara baina yetu katika mpaka wa Namangan a siri kubwa ni amani baina ya wananchi wetu,” amesema Makalla.

Naye Mwenyekiti wa Bunge la Tanzania, Cecilia Paresso alipopewa nafasi ya kuwasalimia wananchi kupitia mkutano huo amesema kazi kubwa ya Bunge ni kusimamia na kuishauri Serikali na kazi hiyo wataifanya kwa uweledi.

Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi Mkoa wa Arusha, Thomas Ole Sabay amesema mkoa huo umepewa Sh4 trilioni kwa ajili ya miradi ya maendeleo.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *