Dar es Salaam. Majina mengi ya wasanii si yale yaliyopo katika vyeti vyao vya kuzaliwa. Asilimia kubwa hujipachika majina mapya ambayo wanaona yanaendana na kile wanachofanya katika sanaa.

Hata hivyo, wapo ambao waliamua kutumia majina waliyopewa na bibi zao tangu wakiwa wadogo, na sasa wanayatumia katika muziki na kuwatambulisha vizuri. Baadhi yao ni hawa:

FAC 05

1. Nandy: Mwanzilishi huyu wa The African Princess Label iliyomtoa kimuziki Yammi, jina analolitumia katika muziki linatokana na Nandera, ambalo alipewa na bibi yake upande wa mama. Pia Nandera ndilo lilikuwa jina la bibi yake huyo. Ni Nandy ambaye anaelekea kutimiza miaka 10 tangu alipotoka rasmi kimuziki kupitia wimbo wake, Nagusagusa (2016) uliotayarishwa na Emma The Boy chini ya Tanzania House of Talent (THT).

FAC 02

2. Shetta: Ni bibi yake ndiye aliyempa jina la Shetta tangu akiwa mdogo. Maana ya jina hilo ni samaki mjanja kwa lugha ya kabila lao la Wangoni. Alianza muziki akitumia jina la Dogo Shetta kabla ya kuondoa neno “Dogo” na kubaki na Shetta. Rapa huyo, ambaye sasa ni meya wa Jiji la Dar es Salaam, alitoka rasmi kimuziki na kibao chake, Nimechokwa (2011) akimshirikisha Belle 9, baada ya kupita Misifa Camp ya Dully Sykes kama dansa wakati huo.

FAC 04

3. Malaika: Wazazi wake walimuita Diana, lakini katika muziki anajiita Malaika, jina alilopewa na bibi yake upande wa mama. Akiwa mdogo, bibi yake alipenda kumuita jina hilo, ndipo akalizoea hadi kuanza kulitumia kwenye muziki. Ikumbukwe Malaika alianza kuvuma kupitia wimbo wa Chege, Uswazi Take Away (2014) aliyoshirikishwa. Baadaye alionyesha uwezo mkubwa kupitia nyimbo zake kama Sare Sare (2015), Zogo (2015) na Rarua Rarua (2016).

FAC 01

4. Mayunga: Mwimbaji huyu ni mshindi wa shindano la Airtel Trace Music Star Africa mwaka 2015 lililojumuisha nchi 12 katika fainali. Jina lake hilo alipewa na bibi yake, na lina maana ya mtembezi au mtu anayependa kutembea. Ni Mayunga ambaye alishirikiana na msanii wa Senegal mwenye makazi yake Marekani, Akon, katika wimbo wake Please Don’t Go Away (2016) uliompa sifa nzuri kimataifa kwa wakati huo.

FAC 03

5. Shilole: Jina hili alipatiwa na bibi yake, na maana yake katika kabila lao la Wanyamwezi ni kioo. Hii ni kutokana na kwamba alipokuwa mdogo, kila alipolia bibi yake alikuwa akimpatia kioo, na pindi alipojiangalia mara moja alinyamaza. Staa huyo alitoka kimuziki na wimbo wake Nakomaa na Jiji (2013) baada ya kuonekana katika video ya wimbo wa 20 Percent, Tamaa Mbaya (2011). Amekuwa pia akitumia jina lake katika biashara zake kama Shilole Entertainment, Shishi Gang na Shishi Food.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *