Katika mkutano huu wa kila mwaka kwa wajumbe wengi vijana, si wa majadiliano pekee bali ni nafasi ya kuhakikisha wanawake hasa vijana wanashiriki kikamilifu katika kutafuta suluhu za changamoto za dunia.
Eunice Kisiwaa Gyan, mwanaharakati kijana mwenye asili ya Ghana na anayeishi hapa Marekani.
Vijana wataka uongozi na hatua halisi
Eunice Kisiwaa Gyan, mwanaharakati kijana mwenye asili ya Ghana na anayeishi hapa Marekani, anasema vijana wanawake hawapaswi kuwa washiriki wa alama tu, bali wanahitaji kuwa sehemu ya uongozi katika masuala muhimu kama katika kila nyanja.
“Hatuko hapa kuwa kama ishara ya mfano tu. Tuko hapa kuzungumzia ushiriki wa wanawake katika amani na usalama, ushiriki wa wanawake katika hatua za tabianchi… kwa sababu bila sisi kizazi kijacho hakiwezi kuendelea kuwepo. Ndoto zenu ni muhimu, maisha yenu ni muhimu na thamani yenu ni kubwa kuliko tu sura nzuri”.”
Gyan anasema kuwa kuwapa nguvu vijana wanawake kuzungumza na kushika nafasi za uongozi ni muhimu katika kujenga jamii jumuishi zenye haki na, haki ya kisheria na hatua zaidi.
Kuongeza uelewa kuhusu mila na vitendo hatarishi
Mshiriki mwingine kijana, ni Taslimat Yusuf kutoka Nigeria, anahudhuria mkutano huo ili kuangazia changamoto zinazoendelea katika jamii yake kama ukeketaji wa wasichana na ukatili wa kijinsia.
Anawakilisha shirika la Shirika la Sauti Moja kwa Ukombozi wa Wanawake na Watoto au One Voice Initiative for Women and Children Emancipation.
Mshiriki wa mkutano wa CSW70 Taslimat Yusuf kutoka Nigeria.
Yusuf anasema manusura wa ukatili katika jamii yake mara nyingi huogopa kuzungumza kutokana na hofu na unyanyapaa, hivyo amesisitiza katika jukwaa hili kwamba kuna haja kubwa ya mifumo madhubuti ya msaada.
“Tunahitaji kuwapa manusura sauti na kuwajulisha kuwa hawako peke yao, wanaonekana na sauti zao zitasikika. Haki lazima itendeke kwao na hii ndio sababu niko hapa kuchagiza uelewa kuhusu ukeketaji, ukatili wa kijinsia na kuona jinsi ambavyo nitaweza kubadilishana mawazona washiriki wengine.”
Serikali zatakiwa kuunga mkono juhudi zilizopo
Taslimat pia anazitaka serikali kushirikiana na mashirika ambayo tayari yanafanya kazi ya kusaidia manusura wa vitendo hivyo badala ya kuanzisha taasisi mpya zinazoweza kurudia kazi zilizopo. Anasema kupanua wigo vituo vya msaada kwa waathirika wa ukatili wa kijinsia kutasaidia waathirika kupata msaada na haki kwa haraka.
Kadri mkutano huo unavyoendelea, wanaharakati vijana wanasema ujumbe wao kwa viongozi ni wazi: ahadi lazima zibadilishwe kuwa hatua halisi ili kuleta maendeleo ya kweli kwa wanawake na wasichana duniani.