Bi. Osowobi amesema hayo jijini New York, Marekani baada ya kupokea tuzo ya uchukuaji wa hatua katika kusongesha Malengo ya Maendeleo Endelevu, SDGs, kufuatia mchango wake wa kusaidia manusura wa ukatili wa kingono na kijinsia kupitia shirika lake aliloasisi la kutokomeza ubakaji liitwalo STER kwa kirefu Stand to End Rape Iniative. Akihojiwa na Idhaa ya Kirusi ya Umoja wa Mataifa mwanaharakati huyo ambaye ni manusura wa ukatili amesema;

 “Ni kwa sababu unapotazama takwimu, ukatili dhidi ya wanawake mara nyingi hutekelezwa na wanaume. Mfano, mvulana anapompeleka msichana kwenye mlo wa jioni na analipia kila kitu. Mwishoni anamwambia ‘twende kwangu.’ Na akisema hapana, wakati alikuwa na matumaini kwa sababu amemununulia mlo, basi anapaswa kuambatana naye hadi nyumbani kwake. Kwa hiyo tusaidie ili watu waone kwamba  unaweza kwenda mlo na mtu, lakini bila matarajio yoyote. Lazima kuweko na ridhaa ya jinsi nyingine kwenye uhusiano wowote au makubaliano ya kujamiiana. Hivyo ni muhimu kujumuisha wanaume kwani siwezi kusema lakini kwa bahati mbayá katika mazingira mengi ya kijamii, wanaume ndio wenye nguvu.”

Akaenda mbali kusisitiza kuwa,

“Wanaume huamua kinachotokea. Kwa hiyo, tusipowapa elimu, basi ukosefu wao wa maarifa kwenye hoja hii hatimaye utakuwa na madhara  usalama na haki za wanawake.”

Alipoulizwa iwapo anaona katika kipindi cha miaka 10 iliyopita kumekuweko na mabadiliko chanya kwenye ushiriki wa wanaume katika kuendeleza na kutetea haki za wanawake, Bi. Osowobi ambaye pia ni mshiri wa tuzo ya Jukwaa la Kimataifa la WanawakeVijana amesema,

“Kumekuwa na ukuaji na maboresho katika suala la mabadiliko au mwelekeo mpya wa kanuni za kijamii, hasa kutokana na uhamasishaji mkubwa uliofanyika. Hivyo basi, sasa kuna wanaume wanaojitambulisha kama wanaharakati wa usawa wa kijinsia. Pia kuna wanaume wanaoongoza na kuhamasisha mipango katika jamii zao au hata katika ngazi ya kitaifa.

Hayo ni mafanikio makubwa. Pia tunao wavulana ambao tumewafundisha kuhusu uanaume chanya na usawa wa kijinsia, na sasa wana uelewa bora wa jinsi ya kuhusiana na wanawake, pamoja na kuheshimu uhuru na haki za wanawake.”

Pamoja na mabadiliko chanya,

“Lakini bado kuna mambo mengi ambayo tunahitaji kubadilisha, kwa sababu kuna baadhi ya mila za kitamaduni ambazo huruhusu kwamba familia inapokuwa na deni kwa familia nyingine, hutumia binti yao kulipa deni hilo kwa sababu familia haiwezi kumudu kulilipa kwa fedha. Hivyo mtoto wa kike anakuwa ndio malipo ya deni. Huo ni utamaduni ambao bado umeenea, na tunajaribu kuubadilisha ndani ya jamii zetu.”

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *