
Siku moja baada ya mkutano wa kiuchumi kati ya Afrika na Ufaransa jijini Nairobi, rais Emmanuel Macron amewasili Ethiopia leo Jumatano, Mei 13, 2026. Atakutana na Waziri Mkuu Abiy Ahmed, wiki chache kabla ya uchaguzi mkuu nchini humo, na pia atatembelea makao makuu ya Umoja wa Afrika.
Imechapishwa:
Dakika 2 Wakati wa kusoma
Matangazo ya kibiashara
Na mwandishi wetu huko Addis Ababa, Marlène Panara
Akipokelewa katika makao makuu ya Umoja wa Afrika, Emmanuel Macron atatoa hotuba leo Jumatano, Mei 13, ikiwa ni mara ya kwanza kwa rais wa Ufaransa. Wakati wa ziara yake ya awali katika makao makuu ya Umoja wa Afrika mwaka wa 2019, alizungumza tu katika mkutano na waandishi wa habari. Pia kwenye ajenda ni mkutano wa pande tatu na Antonio Guterres, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, na Mahmoud Ali Youssouf, Mwenyekiti wa Tume ya Umoja wa Afrika, kujadili migogoro inayokabili bara hilo, ikiwa ni pamoja na hali nchini Mali na vita nchini Sudan. Suala la maendeleo ya nishati mbadala pia litajadiliwa.
Masuala ya kiuchumi
Emmanuel Macron anapanga kujadili masuala ya kiuchumi na Waziri Mkuu wa Ethiopia Abiy Ahmed. Mnamo mwezi Februari, nchi hizo mbili zilisaini makubaliano ya urekebishaji wa deni na mpango mpya wa ufadhili wa euro milioni 81 ili kusaidia mageuzi ya uchumi mkuu yanayoendelea nchini Ethiopia. Kulingana na Wizara ya Fedha ya Ethiopia, ushirikiano wa Ufaransa na Ethiopia sasa unawakilisha zaidi ya euro milioni 600 katika uwekezaji, ambapo zaidi ya euro milioni 300 zimetengwa kwa sekta ya nishati.
Mkutano wa kiuchumi kati ya Afrika na Ufaransa jijini Nairobi, Kenya, pia uliibua swali la ushawishi wa Ufaransa katika Afrika Mashariki na Pembe ya Afrika. Katika upande wa kijeshi, Paris inapanua uwepo wake katika kandi hizi, huku uwepo wake katika nchi za Sahel na Afrika Magharibi ukipungua. Ujumbe wa kijeshi wa Ufaransa umetumwa nchini Ethiopia tangu mwaka 2019. Mojawapo ya misheni zake ni kutoa mafunzo kwa jeshi la majini la Ethiopia, ingawa nchi hiyo haina bandari.
Mkataba wa kijeshi
Tangu 2019, makubaliano ya ushirikiano yaliyosainiwa na Paris yamesimamia mafunzo ya wanajeshi wa Ethiopia na jeshi la Ufaransa. Makubaliano hayo ambayo yalisitishwa katika wiki za mwanzo za vita vya Tigray mwishoni mwa mwaka 2020, yalirejeshwa mapema mwaka 2023, baada ya kusainiwa kwa Mkataba wa Amani wa Pretoria.
Lengo la Ufaransa: kuwa na mshirika katika Mlango wa Bab-el-Mandeb katika Bahari Nyekundu na kushindana na Urusi. Kwa upande wake, jeshi la majini la Ethiopia linanufaika na makubaliano haya kupitia mafunzo ya usalama yanayotolewa na wanajeshi wa Ufaransa, au baharini, ndani ya meli za kivita zenye makao yake Toulon au Brest.
Sébastien Pellissier, afisa wa masuala ya ulinzi katika ubaliozi wa Ufaransa huko Addis Ababa, anahakikisha kwamba makubaliano haya yanaweza kusitishwa tena iwapo kutatokea mgogoro mpya. Katika miezi ya hivi karibuni, mvutano kati ya Eritrea na Ethiopia, ambayo inadai ufikiaji wa bahari kupitia bandari ya Eritrea ya Assab, umeongezeka kwa kasi, na kufanya vita mpya kati ya majirani hao wawili kuwa ya kuaminika zaidi.