Kituo kipya cha mafuta chafunguliwa kuongeza hudumaKituo kipya cha mafuta chafunguliwa kuongeza huduma

Dar es Salaam. Kampuni ya Evosha Energies imepanua mtandao wake wa usambazaji wa mafuta kwa kufungua kituo kipya cha huduma za mafuta katika makutano ya Mbezi Makabe wilayani Ubungo, hatua inayotarajiwa kuboresha upatikanaji wa huduma za mafuta kwa wakazi wa eneo hilo linalokua kwa kasi.

Kituo hicho kipya kilizinduliwa rasmi mwishoni mwa wiki na Mkuu wa Wilaya ya Ubungo, Albert Msando, ambaye alisema uwekezaji huo utasaidia kukidhi ongezeko la mahitaji ya huduma za mafuta kutokana na ukuaji wa haraka wa miji pamoja na kuongezeka kwa shughuli za usafiri katika eneo hilo.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Msando alisema kituo hicho kitasaidia kurahisisha upatikanaji wa mafuta kwa madereva, waendesha bodaboda pamoja na jamii zinazozunguka eneo hilo huku kikichochea shughuli za biashara za ndani.

“Uwekezaji huu ni muhimu kwa sababu unasogeza huduma muhimu karibu zaidi na wananchi na kusaidia shughuli za kiuchumi zinazoendelea katika eneo hili linalokuwa kwa kasi,” alisema.

Mkurugenzi wa Mauzo wa Evosha Energies, Justin Shengelema, alisema kampuni hiyo inalenga kupanua huduma za mafuta zilizo salama, za uhakika na zinazopatikana kwa urahisi katika maeneo mbalimbali ya kimkakati jijini Dar es Salaam.

Alibainisha kuwa kituo hicho cha Mbezi kinatarajiwa kupunguza muda ambao wakazi na madereva hutumia kufuata huduma za mafuta, jambo litakalosaidia kuongeza ufanisi katika shughuli za usafiri na biashara za kila siku.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *