Kocha wa timu ya Taifa ya Uholanzi, Ronald Koeman ametangaza kujiuzulu nafasi yake baada ya timu hiyo kuondolewa na Morocco katika hatua ya 32 Bora ya Kombe la Dunia.

Katika mechi hiyo iliyochezwa Jumatatu, Juni 29, 2026, Uholanzi ilifungwa kwa mikwaju ya penalti 3-2 baada ya timu hizo kutoka sare ya bao 1-1 katika dakika 120.

Koeman mwenye umri wa miaka 63, amesema kuwa ameamua kuwajibika na matokeo yaliyotokea ambayo yamefanya Uholanzi isitimize ndoto.

“Inaumiza kuona kipindi changu na Oranje (Timu ya Taifa ya Uholanzi) unaishia hivi. Wote tulikuwa na ndoto na Kombe la Dunia ambalo tungeandika historia. Hilo halikufanya kazi kwetu.

“Hakuna aliyeumia zaidi kwa hilo kunizidi. Kama Kocha Mkuu, unabeba wajibu huo. Mara zote nilikuwa nafikiria hilo na mara zote ningeendelea kuwaza hilo,” amesema Koeman.

Kupoteza dhidi ya Morocco juzi, kumeibua ukosoaji mkubwa kwa Koeman na baadhi ya nyota wa kikosi cha Uholanzi wakituhumiwa kuiangusha timu hiyo.

“Koeman na nahodha wake Virgil van Dijk wamesaliti kila kitu ambacho timu yetu ya taifa imesimamia kule Monterrey.

“Kwa kuchagua staili ya kujilinda iliyopitiliza, Va Dijk hakuwa imara katika majukumu yake ya kiulinzi wakati wa hatua ya makundi ya Kombe la Dunia,” amesema mwandishi wa habari wa Uholanzi, Valentijn Driessen.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *