
Dar es Salaam. Chuo Kikuu cha Udaktari cha Aga Khan (AKU), kimezindua maktaba ya kisasa katika hospitali ya Aga Khan kwa ajili ya wanafunzi na watafiti.
Uwepo wa maktaba hiyo utawezesha pia hata wagonjwa wanaopata matibabu hospitalini hapo kutembelea ili kujifunza na kupata maarifa.
“Maktaba hii imesheheni vitabu vya kada mbalimbali za udaktari ikiwemo udaktari bingwa na bobezi.”
“Maktaba hii ya kipekee imejengwa katika mazingira ya ndani ya hospitali ili kuwezesha upatikanaji wa taarifa na kujiendeleza kwa madaktari, wanafunzi na wagonjwa,” amesema Mkuu wa Chuo cha Udaktari cha Aga Khan, Profesa Paschal Ruggajo.
Uzinduzi huo umefanywa leo Jumatano, Julai Mosi, 2026 na Rais wa Vyuo vya Aga Khan duniani, Dk Sulaiman Shahbuddin
Kwa mujibu wa Profesa Ruggjo, maktaba hiyo kutapatikana vitabu za kiada, ziada na vile vya maarifa mbalimbali visivyohusiana na udaktari ili muuguzi au mgonjwa apate kusoma.
“Tunaamini elimu, utafiti na huduma bora vinaendana pamoja. Ili ubora uendelee lazima uambatane na kuongeza elimu katika hatua za mbele,” amesema.
Amesema AKU wanafundisha madaktari bingwa ambao muda mwingi wanakuwa wodini, hivyo akiwa katika maeneo hayo anakuwa na fursa ya kwenda katika maktaba kuongeza maarifa.
“Tunaamini elimu bora, utafiti vinaboresha huduma kwa wagonjwa, ndio maana tumeona umuhimu wa kuwa na maktaba hii ambayo tunaizindua leo,” amesema Ruggajo.
Mkutubi Mkuu wa AKU nchini, Dk Jacqline Kiwelu amesema kitengo hicho kinawasaidia wanafunzi kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi wanaosoma udaktari, uuguzi na ukunga.
“Kulikuwa na maktaba kabla ya hii, lakini ilikuwa eneo finyu haikuweza kusaidia kufanya kazi vizuri na hata wanafunzi kusoma kwa umahiri. Lakini kwa sasa hivi tumepata sehemu kubwa ya kufanya kazi,” amesema.
Dk Kiwelu amesema katika maktaba hiyo kuna sehemu maalumu ya wanafunzi kujisomea na kufanya majadiliano mbalimbali ya kimasomo.