BEKI wa Azam FC, Nathaniel Chilambo, amempa sifa kocha mkuu wa timu hiyo, Florent Ibenge namna anavyowapa nafasi wachezaji na imekuwa moja ya sababu ya kiwango chake kuwa bora zaidi msimu huu.
Chilambo ambaye amekuwa mmoja wa mabeki waliotumika mara kwa mara na Azam FC katika mashindano mbalimbali msimu huu, amesema ujio wa Ibenge umeongeza ushindani ndani ya kikosi na kumfanya kila mchezaji kupambana ili kuhakikisha anakuwa sehemu ya kikosi cha kwanza.
Beki huyo amesema tofauti kubwa aliyoiona chini ya kocha huyo ni kwamba hakuna mchezaji anayehakikishiwa nafasi kikosini, jambo ambalo limewafanya wote kufanya kazi kwa bidii mazoezi na kila wanapopewa nafasi ya kucheza.
“Nashukuru Mungu kwa kumaliza msimu vizuri, hilo ni jambo kubwa kwangu kama mchezaji. Lakini pia nimshukuru kocha kwa kutusaidia sisi wachezaji kwa sababu kitendo cha kutupa nafasi kila mmoja ni jambo kubwa sana. Hilo limeongeza ushindani ndani ya kikosi na kila mmoja anapambana kuonyesha uwezo wake,” amesema Chilambo.
Beki huyo amesema ushindani huo umechangia yeye kurejea kwenye kiwango bora zaidi tofauti na misimu miwili iliyopita alipokuwa bado anajitafuta baada ya kutua Azam.