
Dar es Salaam. Utafiti mpya umebaini kuwa kula vyakula vilevile mara kwa mara pamoja na kudumisha kiwango kinachofanana cha kalori kila siku, kunaweza kusaidia mtu kupunguza uzito kwa ufanisi zaidi kuliko kula aina nyingi tofauti za vyakula.
Aidha, matokeo ya utafiti huo yanaonyesha kuwa hata wale wanaokula kalori nyingi zaidi mwishoni mwa wiki wanaweza kufanikisha kupunguza uzito kuliko ilivyodhaniwa hapo awali.
Katika miaka ya hivi karibuni, watu wengi wameanza kutumia dawa za kupunguza uzito kama zile zinazojulikana kwa jina la GLP-1.
Hata hivyo, bado kuna watu wengi wanaopendelea njia za asili kama lishe bora au mifumo ya kula iliyopangwa vizuri ili kudhibiti uzito wao.
Wataalamu wanasema kuwa kubadilisha tabia za ulaji bado ni hatua ya kwanza inayopendekezwa kwa watu wengi wanaotaka kupunguza uzito.
Utafiti huu mpya uliochapishwa katika jarida la Health Psychology uliangalia kwa kina tabia za ulaji wa watu 112 waliokuwa na uzito kupita kiasi au unene uliokithiri.
Washiriki walikuwa na wastani wa umri wa miaka 53 na walikuwa wamejiunga na programu maalum ya kupunguza uzito inayotumia mbinu za kitabia. Kila mshiriki alitakiwa kurekodi kila alichokula kila siku kupitia programu ya simu, pamoja na kufuatilia uzito wake mara kwa mara.
Watafiti walichambua taarifa hizo kwa kuzingatia mambo mawili muhimu. Kwanza walichunguza jinsi kiwango cha kalori kinavyobadilika siku hadi siku kwa kila mshiriki. Pili waliangalia ni mara ngapi washiriki walikula vyakula au milo ileile mara kwa mara badala ya kubadilisha kila siku.
Matokeo yalionyesha kuwa watu waliokuwa na uthabiti mkubwa katika kiwango cha kalori walichokula kila siku walipata mafanikio zaidi katika kupunguza uzito.
Ilibainika kuwa kila ongezeko la kalori 100 katika mabadiliko ya kila siku lilihusishwa na kupungua kwa kiwango cha uzito kinachopotea kwa takribani asilimia 0.6 katika kipindi cha utafiti.
Zaidi ya hapo, watafiti waligundua kuwa kurudia vyakula vilevile mara kwa mara kulikuwa na mchango mkubwa katika kupunguza uzito.
Washiriki waliokula zaidi ya asilimia 50 ya vyakula vilevile walipoteza wastani wa asilimia 5.9 ya uzito wa miili yao, ikilinganishwa na asilimia 4.3 kwa wale waliokuwa na mlo wenye mchanganyiko mkubwa wa vyakula tofauti.
Kilichoshangaza
Ugunduzi mwingine uliowashangaza watafiti ni kwamba washiriki waliorekodi ulaji wa kalori nyingi zaidi mwishoni mwa wiki kuliko siku za kawaida pia walionekana kupunguza uzito zaidi.
Hili linapingana na dhana iliyokuwa imezoeleka kuwa mtu anapaswa kula kwa kiwango kinachofanana kila siku bila kuongeza mwishoni mwa wiki.
Watafiti wanaeleza kuwa huenda ulaji wa kalori nyingi mwishoni mwa wiki unasaidia kupunguza hisia za kujinyima kupita kiasi. Hali hii inaweza kuwasaidia watu kudumisha nidhamu ya lishe yao katika siku za kawaida za wiki, na hivyo kufanikisha mpango wao wa kupunguza uzito kwa ujumla.
Kwa mujibu wa wataalamu, kula vyakula vilevile mara kwa mara kunaweza kupunguza mzigo wa kufanya uamuzi kila siku kuhusu chakula.
Badala ya kufikiria kila mara ni chakula gani cha kula, mtu anakuwa na utaratibu unaojirudia ambao unarahisisha kufuata mpango wa lishe.
Hali hii pia husaidia katika kufuatilia kalori kwa urahisi na kupunguza uwezekano wa kufanya uamuzi usio sahihi wa kula.
Hata hivyo, watafiti wanatahadharisha kuwa matokeo haya yanaonesha uhusiano tu na si sababu kamili ya kupunguza uzito.
Sababu nyingine kama nidhamu binafsi, motisha, na mazingira ya mtu zinaweza pia kuwa na mchango mkubwa katika mafanikio ya kupunguza uzito.
Kwa ujumla, utafiti huu unaonesha kuwa uthabiti katika tabia za ulaji unaweza kuwa muhimu zaidi kuliko kubadilisha vyakula mara kwa mara.
Kuwa na milo ya kawaida inayojirudia na kudhibiti kiwango cha kalori kila siku kunaweza kusaidia kujenga tabia endelevu za kiafya.
Matokeo haya yanaweka wazi kuwa wakati mwingine urahisi na utaratibu vinaweza kuwa silaha bora katika safari ya kupunguza uzito.
Badala ya kufuata mifumo migumu ya lishe, kujenga mfumo rahisi unaojirudia kunaweza kuwa njia yenye ufanisi zaidi kwa watu wengi.
Makala hii imetafsiriwa kutoka tovuti ya Medical News Today.