
TIMU ya Mashujaa tayari imemalizana na kocha, Amani Josiah kwa ajili ya kukinoa kikosi hicho msimu ujao unaotarajia kuanza Agosti 14, 2026, akichukua mikoba ya Jamhuri Kihwelo ‘Julio’ aliyeisaidia kumaliza nafasi ya 11 na pointi 33 msimu uliopita.
Josiah anakwenda kujiunga na Mashujaa akitokea Dodoma Jiji ambako aliisaidia timu hiyo kumaliza nafasi ya tisa na pointi 35, huku wakipigwa chini makocha wengine ambao walikuwa wanazungumza na timu hiyo ambao ni Fikiri Elias (Coastal Union), Mecky Maxime (hakumaliza msimu na Mbeya City) na Zuber Katwila (aliyeipandisha Geita Gold).
Chanzo cha ndani kutoka Mashujaa kilisema tayari kocha huyo ameshajiunga na timu hiyo na jambo lilobaki ni kutambulishwa tu ambalo litafanyika muda wowote .
“Kesho Jumanne (leo) anaweza akatambulishwa kocha, maana tayari ameishajiunga na kambi bado tu kuanza majukumu yake na uongozi kuweka wazi ujio wake na kambi kuanza rasmi,” kilisema chanzo hicho na kuongeza;
“Wachezaji wapya ambao watajiunga kambini kesho Jumatano ni Hassan Kabunda kutoka Namungo FC, Abdallah Mfuko kutoka TRA United, wengine bado tunazungumza nao hatujakamilisha usajili,” kilisema chanzo hicho.