Katika kura ya kihistoria iliyopigwa Umoja wa Mataifa siku ya Alkhamisi, profesa wa sheria wa Kenya Phoebe Okowa alichaguliwa kuwa jaji wa Mahakama ya Kimataifa ya Haki (ICJ), akiibuka mshindi kwenye ulingo wa ushindani wa wagombea wa Kiafrika baada ya mfululizo wa raundi za kupiga kura zilizokuwa na mvutano katika Baraza Kuu na Baraza la Usalama.

Uchaguzi huo ulishuhudia Okowa akishindana dhidi ya wagombea kutoka Nigeria, Sierra Leone, na Ghana katika kinyang’anyiro kilichochukua muda mrefu.

Baada ya raundi kadhaa zisizo na hitimisho ambazo hazikutoa wingi unaohitajika katika vyombo vyote viwili vya Umoja wa Mataifa, wagombea Paul Kuruk wa Ghana na Dkt. Olufemi Elias wa Nigeria walijiondoa kwenye orodha ya wagombea.

Raundi ya mwisho ya mchuano huo iliwakutanisha Okowa dhidi ya Charles Jalloh wa Sierra Leone, huku mgombea wa Kenya akipata kura 106 dhidi ya 79 za Jalloh katika Baraza Kuu na ushindi mwembamba wa 8-7 katika Baraza la Usalama.

Rais wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa Annalena Baerbock alitangaza rasmi kwamba “Phoebe Okowa wa Kenya amepata wingi kamili katika vyombo vyote viwili” na kwa hivyo amechaguliwa rasmi.

Okowa anamrithi Jaji Abdulqawi A. Yusuf, ambaye alijiuzulu kuanzia Septemba 30, 2025.

Muhula wake wa kuhudumu katika Mahakama ya Haki ICJ unaanza mara moja na utaendelea hadi Februari 5, 2027, akikamilisha muda uliobaki wa mtangulizi wake katika chombo hicho kikuu cha mahakama cha Umoja wa Mataifa, ambacho mara nyingi huitwa “Mahakama ya Dunia”…/

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *