
Nchini Senegal, mashirika kumi na tano yanayotetea haki za wanawake yanamtaka Rais Bassirou Diomaye Faye kutekeleza maneno kwa vitendo, baada ya kutangaza kujikita kwa usawa wa kijinsia na kutetea haki za wanawake katika Umoja wa Mataifa siku ya Jumatatu, Septemba 22. Wanatoa wito wa mageuzi madhubuti.
Imechapishwa:
Dakika 1 Wakati wa kusoma
Matangazo ya kibiashara
Na mwandishi wetu wa habari huko Dakar, Léa-Lisa Westerhoff
Kufikia usawa wa kijinsia “kamili”, lakini pia kuwawezesha wanawake na kupambana na unyanyasaji wa kijinsia… Ahadi zilizotolewa na Bassirou Diomaye Faye kwenye jukwaa la Umoja wa Mataifa huko New York zimezingatiwa.
Dk. Ndeye Khadi Babou, ambaye anaratibu shirika la wanawake nchini Senegal, ananyoonyesha kidole pengo kati ya matamshi na ukweli. “Katika Umoja wa Mataifa, alisisitiza haja ya uwakilishi mkubwa wa wanawake katika nafasi za maamuzi. Lakini katika serikali zake mbili zilizopita, tumekuwa na chini ya asilimia 15 ya wanawake, ikiwa ni pamoja na nyadhifa zote za uteuzi,” anabainisha.
Anakumbusha hali mbaya ya haki za wanawake nchini Senegal. “Tulianza mwaka na msichana mdogo ambaye alijiua ili kutoroka ndoa ya kulazimishwa, au wanawake waliouawa na waume zao kwa sababu hawakuweza kuandaa chakula… Tumekuwa na angalau kesi mbili kwa mwezi tangu mwezi Januari,” daktari analalamika.
Jukwaa linalomtaka rais kutimiza ahadi zake za kampeni
Pamoja na mashirika mengine 14 yanayotetea haki za wanawake, Aminata Libain Mbengue ametia saini jukwaa la kumtaka rais kutimiza ahadi zake za kampeni. “Mgombea Diomaye, katika sera zake, aliahidi kubadili sheria nyingi za kibaguzi: kuhakikisha kuwa mamlaka ya wazazi yanashirikiwa, ili kubatilisha umri halali wa kuolewa kwa wasichana, ambao ni miaka 16, na tunajua kwamba hii ni kikwazo kwa haki za wasichana, pamoja na kufunguliwa kwa uchunguzi wa DNA katika kesi za ubakaji,” anabainisha.
Pia bado kuna haki ya kutoa mimba, ambayo haipo nchini Senegal, hata katika kesi za ubakaji, ingawa Dakar iliidhinisha Itifaki ya Maputo, ambayo inaidhinisha utoaji mimba, zaidi ya miaka 20 iliyopita.