Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa limepiga kura kuunga mkono azimio la Marekani siku ya Alhamisi la kuondoa vikwazo dhidi ya Rais wa Syria Ahmed al-Sharaa, kabla ya ziara yake ya Ikulu wiki ijayo. 

Azimio hilo, lililoidhinishwa na wanachama 14 wa baraza la usalama hapo jana limesema baraza hilo linaamua kwamba Ahmed al-Sharaa…na waziri wa mambo ya ndani Anas Hasan Khattab wameondolewa kwenye orodha ya vikwazo vya kundi la dola la kiislamu ISIL na Al-Qaida. China ilijizuia kulipigia kura azimio hilo.

Kuondolewa rasmi kwa vikwazo dhidi ya Sharaa ni ishara kubwa kwani viliondolewa kila wakati alipohitaji kusafiri nje ya Syria katika nafasi yake kama kiongozi wa nchi hiyo. Kufungiwa kwa mali na vikwazo vya silaha pia vitaondolewa.

Hatua hiyo ilipongezwa na Syria, huku waziri wa mambo ya nje Asaad al-Shaibani akiandika katika mtandano wa  kijamii wa X: “Syria inatoa shukrani zake kwa Marekani na mataifa rafiki kwa msaada wao kwa Syria na watu wake.”

Rais wa Marekani Donald Trump atamkaribisha Sharaa kwa mazungumzo mnamo Novemba 10, baada ya kusema kwamba mpiganaji huyo wa zamani wa jihadi amepata “maendeleo mazuri” kuelekea kuleta amani katika nchi yake iliyokumbwa na vita.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *