Vijana wengi katika jiji la Tanga wamejikuta wakishindwa kufikia matarajio yao katika maisha kuto­kana na kukosa fursa. Hii imesaba­bisha wengi kujikita kwenye kazi zisizo rasmi, ukulima mdogo na shughuli za uvuvi zisizokuwa ende­levu.

Aidha, ufikiaji mdogo wa mifumo ya kifedha au mafunzo ya ujasiria­mali, uwekaji wa akiba kwa vijana hao vilionekana kuwa changamo­to na hivyo kuwafanya kushindwa kutekeleza shughuli endelevu za kiuchumi.

Pia, maelfu ya vijana katika jiji hilo wanakabiliwa na changamoto nyingine ikiwemo; ukosefu wa ajira, upatikanaji mdogo wa mikopo na ukosefu wa mawazo ya kibiashara ambayo yanaweza kuwasaidia kuto­kutegemea kuajiriwa. Katika jamii ambapo upatikanaji wa mitaji mara nyingi unarudisha nyuma maende­leo ya vijana wengi, Tanga nayo ni sehemu yenye changamoto hiyo.

Hapa ndipo unapoingia Mradi wa Mabadiliko ya Fikra na Ujasiriama­li ambao ni sehemu ya awamu ya kwanza ya programu ya TangaY­etu iliyoongozwa na Reconstructed Living Lab (RLabs). Mradi huu len­go lake sio tu kutoa mafunzo kwa vijana katika ujasiriamali, lakini pia kubadilisha jinsi wanavyojiona, kufikiri na kutumia uwezo wao.

Mbinu hii ilianza na utafiti wa kimsingi wa kutathmini fursa za biashara zinazofaa kwa vijana. Kisha zikaja warsha za uongozi za GROW, kambi za mafunzo ya ujasiri­amali, mafunzo ya ujuzi wa kidijitali na vipindi vya mafunzo ya kuweka na kukopa kwa vijana.

Katika jamii zilizofikiwa na mradi huu, kuliundwa vikundi vya kuwe­ka na kukopa vya kijamii kama vile Karange One na TUNDAUWA. Lengo lilikuwa ni kujenga mifumo ya kifed­ha inayoongozwa na kumilikiwa na vijana.

TUNDAUWA ilivyoleta uhuru wa kifedha kwa vijana katika ngazi ya jamii

Umoja wa Vijana TUNDAUWA ni kikundi cha kuweka na kukopa cha vijana chenye wanachama 21 waki­jumuisha wanawake 16 na wanau­me watano ambao wameunganish­wa na dhamira ya pamoja ya ukuaji wa kifedha na kusaidiana. Kupitia kikundi hicho, wanachama huchan­gia mapato yanayotokana na kilimo, uvuvi na ujasiriamali.

Fedha hizi hutolewa kwa njia ya mkopo ili kuwasaidia wanachama kuwekeza katika miradi kama vile kilimo cha mihogo na mabwawa ya samaki. Mbinu hii inasisitiza uthabiti, uaminifu na mtaji wa jamii.

“Hii ni zaidi ya akiba bali ni kuten­geneza fursa za kuwekeza katika siku zijazo. Jambo muhimu katika mpango huu ni dhana ya mabadi­liko ya mawazo,” anasema Muweka Hazina wa TUNDAUWA, Rajabu S. Rajabu.

“Kikundi hiki kilianzishwa baada ya mafunzo yaliyotolewa chini ya TangaYetu kwani kabla ya ujio wa programu hiyo hatukujua tuanzie wapi,” anasema Time Khamisi Sele­mani, mwanachama wa TUNDAU­WA.

Mwezeshaji na Msimamizi wa Mradi, Halima Ally Bughe anaeleza jinsi washiriki walivyojifunza kuba­dilisha mapato ya kawaida kuwa uwekezaji mkubwa. “Tuliwafundi­sha kuweka akiba kidogo kama Sh 100 na sasa wanakuza mitaji yao na kujitegemea.”

Wanachama wa kikundi cha TUNDAUWA wakiwa katika kikao cha kujadili maendeleo, ushirikiano na uwezeshaji wa vijana wa kikundi hicho.

Mwenyekiti wa kikundi cha TUNDAUWA, Rashid Khamisi Ibra­him amesisitiza azma ya kikundi hicho kwa kusema kuwa, “Tunataka kuongeza miradi kama vile kilimo cha mihogo na ufugaji wa samaki. Mawazo haya yanaweza kubadili­sha kikundi chetu na jamii nzima.”

Karange one: Mhimili wa uwezesha­ji wa kifedha kwa vijana

Karange One ni kikundi cha aki­ba na mikopo chenye wanachama wenye umri kati ya miaka 18 hadi 30. Kupitia shughuli za kiuchumi, kikundi hicho kimeonyesha hali ya kujitegemea na ustadi, kuunganisha rasilimali ili kusaidia matarajio ya mtu binafsi na ya pamoja.

Kama vilivyo vikundi vingine, Karange One inatumia njia za michango ya wanachama ambapo michango ya kila wiki ya wanacha­ma inawawezesha kupata mikopo ambayo wanaitumia katika kupanua biasha­ra zao na kukidhi mahitaji ya familia. “Nil­itumia mkopo wa kikundi kujen­ga nyumba ya kisasa na mkopo mwingine ulinisaidia kuanzisha kikundi kingine cha Kijibweni One,” anasema Jafari Shali Rashidi, kati­bu wa kikundi.

Kwa Asia Mmaka Ramadhani ambaye ni Mweka hazina wa kikundi, Karange One ni zaidi ya pesa. “Nguvu zetu ziko katika umo­ja. Kwa pamoja, tunaweka akiba leo ili kujenga usalama wa kesho. Cho­chote kinachotokea katika maisha tunaweza kusaidiana wenyewe kwa wenyewe.”

Wanachama kama Fatuma Mwi­dadi Gau waligeuza mikopo midogo kuwa miradi ya kujiingizia kipato. Alinunua friji na kuanza kutengene­za na kuuza aiskrimu na juisi. Ami­na Ally, mwanachama mwingine, alitumia mtaji wake kupanua duka lake na kusomesha watoto wake. “Kikundi hiki kimekuwa cha kubad­ilisha maisha,” anasema Amina.

Mafanikio hupimwa kwa matokeo

Mbali na faida za kifedha, mafan­ikio makubwa zaidi yamekuwa kati­ka kubadilisha mawazo na mitaza­mo. Kilichoanza kama vipindi vya mafunzo vilibadilika na kuwa shu­ghuli za uchumi. Vikundi ambavyo hapo awali vilitegemea misaada kutoka nje sasa vinajenga uthabi­ti wao wenyewe, kupitia michango midogo midogo ya wanachama wake.

Takwimu zinaonyesha kuwa zaidi ya vijana 1,036 walifikiwa, mamia ya biashara ndogo zilianzishwa, mael­fu ya shilingi za Kitanzania ziliingiz­wa katika mzunguko kama mikopo ya vikundi. Hizi sio tu takwimu za kwenye makaratasi, bali ni ishara ya ujenzi wa uchumi imara na ende­levu kwa jamii hizo.

Mafanikio ya Karange One na TUNDAUWA yanatoa taswira yenye nguvu kwamba maendeleo ya kiu­chumi huanza na kujiamini na kati­ka uwezo wa pamoja wa jamii. Hili ni funzo kwamba mifumo ya kifedha sio lazima iwe na sheria na taratibu nyingi ili kuwa na ufanisi bali inat­akiwa ijengwe katika uaminifu.

Programu ya TangaYetu katika awamu yake ya pili, mfumo wake wa uwezeshaji kwa vijana unatoa funzo ambalo linatakiwa kuigwa katika miji yote ya Afrika la kuwawezesha vijana si tu kwa ujuzi, lakini kwa mifumo na nafasi ya kustawi.

“Vijana wanapokuwa na vifaa, ujuzi na maono ya pamoja, wanafa­nya mengi zaidi ya kukuza biasha­ra,” anasema Halima msimamizi wa mradi kutoka RLabs.

Programu ya TangaYetu inafadhi­liwa na Fondation Botnar na inate­kelezwa na kampuni ya INNOVEX Development Consulting Limited kwa kushirikiana na Halmashauri ya Jiji la Tanga

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *