Kadiri uchumi wa Uingereza unavyozidi kulegea na kuporomoka, takribani robo ya wazazi wenye ajira nao wanalazimika kutafuta msaada wa chakula cha bure kutoka mashirika ya hisani.

Kwa mujibu wa Pars Today, hali mbaya ya kiuchumi nchini Uingereza ikiendelea imepelekea kuongezeka kwa idadi ya watu wanaotafuta chakula cha bure. Matokeo ya uchunguzi wa hivi karibuni yanaonyesha kuwa mamia ya maelfu ya wazazi wenye ajira nchini Uingereza wamelazimika kutegemea mashirika ya hisani au benki za chakula ili kupata mahitaji ya familia zao. Ripoti hizi, zilizotolewa na taasisi ya ‘The Felix Project’, zinaonyesha kuwa kati ya kila wazazi wanne wenye kazi, mmoja huenda mara kwa mara, kila wiki moja au mbili, katika mashirika ya hisani kwa msaada.

Hali ya kiuchumi nchini Uingereza inazidi kuwa mbaya na imepelekea kuongezeka kwa umasikini pamoja na kupanuka kwa pengo la kitabaka. Sababu kuu zinazochangia hali hii ni kujiondoa kwa Uingereza kutoka Umoja wa Ulaya (Brexit), gharama za vita vya Ukraine, migawanyiko ya ndani, na mazingira yasiyo thabiti ya kisiasa na kiuchumi katika nchi nyingi za Ulaya. Hali hii imeifanya mashua ya uchumi wa Uingereza kuyumba katikati ya mawimbi makali, ikionyesha jinsi upepo wa kisiasa na kiuchumi wa bara la Ulaya unavyotikisa safari yake.

Moja ya matatizo makubwa yanayokabili familia za Uingereza ni kuongezeka kwa mfumuko wa bei, na hatimaye kuzuka kwa mgogoro wa gharama na kupanda kwa matumizi ya maisha. Kwa kuongezeka kwa kiwango cha mfumuko wa bei, wananchi wanakabiliwa na kupanda kwa bei za bidhaa na huduma muhimu kama vile chakula, makazi, nishati na usafiri. Hali hii imefanya familia nyingi kushindwa kutimiza mahitaji yao ya msingi. Miongoni mwao, wazazi wenye ajira ambao hapo awali waliweza kwa namna fulani kukabiliana na gharama za maisha, sasa si tu kwamba hawawezi kuhakikisha usalama wa chakula kwa familia zao, bali mara nyingi wamelazimika kukimbilia mashirika ya hisani na benki za chakula ili kupata chakula cha familia zao.

Hali hii, hususan kwa kuanza kwa misimu ya baridi, imekuwa mbaya zaidi. Kwa sababu katika miaka ya hivi karibuni gharama za nishati pia zimepanda kwa kiwango kikubwa nchini Uingereza. Vita vya Ukraine na vikwazo dhidi ya Russia, hasa katika sekta ya nishati, vimesababisha hata nchi za Ulaya zenyewe kukumbwa na matatizo ya kupata mafuta ya kutosha. Matokeo yake, gharama za nishati katika bajeti za familia zimekuwa juu kiasi kwamba familia nyingi hulazimika kuchagua kati ya kununua chakula au kulipa gharama za kupasha joto nyumba zao.

Kwa hakika, vita vya Ukraine si tu vimeathiri moja kwa moja bei ya nishati barani Ulaya, bali pia matatizo ya mnyororo wa usambazaji na upungufu wa malighafi yamesababisha kupanda kwa bei katika sekta nyingi za viwanda. Uingereza, ambayo ilijulikana kama moja ya nchi zinazotegemea uagizaji wa nishati kutoka Russia na Ukraine, baada ya kupita miaka kadhaa tangu kuanza kwa vita vya Ukraine bado inakabiliwa na mgogoro mkubwa katika uwanja huu. Mgogoro huu wa nishati, sambamba na kupanda kwa gharama za bidhaa nyingine, umeweka shinikizo kubwa zaidi kwa familia.

Kwa upande mwingine, takwimu zilizotolewa zinaonyesha kuwa kiwango cha mfumuko wa bei nchini Uingereza katika miaka ya hivi karibuni kimefikia kiwango cha juu kabisa. Kuongezeka huku kwa mfumuko wa bei kumesababisha nguvu ya ununuzi ya familia nyingi kupungua. Gharama za kila siku, ikiwemo chakula, usafiri na hata kodi ya nyumba, zimepanda kwa viwango vya juu sana. Katika mazingira haya, familia hulazimika kutafuta chaguo nafuu zaidi au kutegemea misaada ili kukidhi mahitaji yao ya kila siku.

Udhaifu katika sera za kiuchumi na kijamii za serikali ya Uingereza pia ni miongoni mwa sababu muhimu za mgogoro huu. Wataalamu wengi wanaamini kuwa sera za kiuchumi za Uingereza, hususan katika eneo la kusaidia tabaka la kipato cha chini na wanyonge, hazijapangwa ipasavyo. Kupunguzwa kwa misaada ya kijamii na mipango ya ulinzi wa kijamii ambayo hapo awali ilikuwepo, kumesababisha familia nyingi zaidi kukumbwa na matatizo ya kiuchumi.

Umasikini London

Kwa upande mwingine, baadhi ya sera za kiuchumi kama vile kuongeza kodi au kupunguza matumizi ya umma zimeweka shinikizo kubwa zaidi kwa tabaka la kati na la chini katika jamii. Katika hali hii, familia hulazimika kutegemea mashirika ya misaada au hisani ili kupata chakula kwa watoto wao, na hali ya kutoridhika kijamii imeongezeka. Katika muktadha huu, wataalamu wengi wameonya kuhusu kuongezeka kwa pengo la kitabaka pamoja na kuongezeka kwa hali ya kutokuwa na usalama nchini Uingereza.

Ingawa mgogoro wa kiuchumi wa Uingereza umeathiri sana wazazi wenye ajira, hali hii haijabakia tu ndani ya nchi hiyo. Nchi nyingine za Ulaya pia zinakabiliwa na changamoto zinazofanana. Hususan katika nchi za kusini mwa Ulaya kama Hispania na Ugiriki, kiwango cha juu cha ukosefu wa ajira na gharama kubwa za maisha, sambamba na mgogoro wa kiuchumi wa dunia, vimeweka shinikizo kubwa kwa familia. Katika nchi nyingine kama Ufaransa na Italia, licha ya kuwepo kwa msaada wa kijamii kiasi, familia bado zinakumbwa na matatizo ya kiuchumi kutokana na mfumuko wa bei na kupanda kwa gharama za maisha. Mgogoro huu si tu umeongeza ukosefu wa usawa wa kijamii, bali pia umeathiri moja kwa moja ubora wa maisha ya wananchi katika nchi hizi.

Kuendelea kwa vita vya Ukraine na kuongezeka kwa gharama za kijeshi na kiusalama katika nchi za Ulaya, hususan katika miaka ya hivi karibuni, pamoja na kuongezeka kwa migawanyiko ya ndani ya vyama na makundi ya kisiasa katika baadhi ya nchi za Ulaya kama Ufaransa na Uingereza, na pia mabadiliko ya sera za kijamii na za ulinzi wa jamii, kumesababisha kiwango cha maisha, hasa miongoni mwa tabaka la kati na wanyonge, kushuka. Hali hii imeongeza mahitaji ya msaada wa chakula na huduma za kijamii.

Katika mazingira haya, iwapo serikali hazitaweza kusimamia mgogoro huu kwa ufanisi, huenda hali ya kiuchumi ya nchi mbalimbali za Ulaya ikaelekea kuzorota zaidi.

Kama ambavyo viongozi wa Ulaya pia wameonya kuhusu mgogoro huu. Christine Lagarde, Rais wa Benki Kuu ya Ulaya, amesema: ‘Iwapo serikali hazitaweza kusimamia mgogoro wa kiuchumi, kiwango cha kutokuwa na usawa wa kijamii barani Ulaya kitaongezeka kwa kiasi kikubwa.’ Vilevile Josep Borrell, Kamishna wa Sera za Kigeni wa Umoja wa Ulaya, amebainisha kwamba mgogoro wa nishati unaotokana na vita vya Ukraine sambamba na migogoro ya kiuchumi ya ndani unaweza kusababisha kuongezeka kwa hali ya kutoridhika kijamii na hata kuyumbisha uthabiti wa kisiasa barani Ulaya, ameonya kuhusu kuendelea kwa hali hii.

Hatimaye, mgogoro huu si tu kama changamoto ya kiuchumi, bali pia kama mgogoro wa kijamii unaohitaji uangalizi na hatua za haraka. Hivyo basi, inaonekana kwamba kuongeza msaada kwa tabaka zilizo hatarini, kuimarisha sera za kiuchumi endelevu na kuunda mifumo ya ulinzi wa kijamii ili kupunguza shinikizo kwa familia za tabaka la kati na wanyonge, kunaweza kuzuia kuzorota zaidi kwa hali ya kiuchumi na kupunguza pengo la kijamii. Vinginevyo, kuongezeka kwa mvutano wa kijamii na hali ya kutoridhika kutageuka kuwa tatizo kubwa nchini Uingereza.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *