Viongozi wa Kiafrika na wa kimataifa waliokutana mjini Lomé wamekubaliana kuimarisha na kuunganisha juhudi za upatanishi ili kumaliza mzozo katika eneo la mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC). Mkutano huo umeidhinisha nafasi ya kiungo ya upatanishi unaoongozwa na Togo chini ya mamlaka ya Umoja wa Afrika (AU), kama mhimili mkuu wa kusukuma mbele mchakato wa amani.

Makubaliano hayo yalifikiwa mwishoni mwa mkutano wa siku mbili wa ngazi ya juu uliofanyika Ijumaa na Jumamosi, ukiongozwa na Faure Essozimna Gnassingbé, rais wa Baraza la Jamhuri ya Togo na mpatanishi wa AU katika mgogoro wa Ukanda wa Maziwa Makuu.

Washiriki walizihimiza pande zote kuharakisha utekelezaji wa kwa dhati wa makubaliano ya amani yaliyopo, na kuweka mbele suluhu za kisiasa badala ya kukwama katika mapambano ya kijeshi.

Taarifa ya mwisho ya mkutano ilibainisha umuhimu wa kuwa na mwelekeo mmoja, uratibu thabiti na ulinganifu kati ya juhudi za amani za Kiafrika, kikanda na kimataifa, ili kuepusha mipasuko ya kimkakati inayoweza kuhatarisha uthabiti wa eneo la mashariki mwa DRC.

Mkutano huo uliidhinisha rasmi muundo mpya wa mfumo wa upatanishi, ikiwemo kuanzishwa kwa Sekretarieti Huru ya Pamoja itakayolisaidia Baraza la Wapatanishi la AU, ambalo linajumuisha marais wastaafu kutoka Nigeria, Kenya, Jamhuri ya Afrika ya Kati, Botswana na Ethiopia.

Viongozi walithibitisha tena kuunga mkono mchakato wa Doha kati ya serikali ya Kongo na kundi la waasi la AFC/M23, wakizitaka pande hizo kurejea mezani bila kuchelewa ili kukamilisha mazungumzo kuhusu itifaki sita zilizobaki ndani ya mfumo mpana wa makubaliano ya amani uliopitishwa mwaka 2025.

Mapigano katika mashariki mwa DR Congo yameongezeka katika miezi ya hivi karibuni licha ya kile kinachoitwa makubaliano ya amani yaliyosainiwa Desemba 4 mjini Washington kati ya Rais wa Kongo Félix Tshisekedi na Rais wa Rwanda Paul Kagame, yaliyolenga kusitisha vita mashariki mwa nchi hiyo. Wachambuzi walitafsiri makubaliano hayo kama sehemu ya mpango wa Rais wa Marekani Donald Trump wa kupora rasilimali muhimu za madini kutoka mashariki mwa DRC.

Kundi la waasi la M23 linaendelea kudhibiti maeneo makubwa mashariki mwa Kongo, yakiwemo miji mikuu ya mikoa ya Goma na Bukavu, ambayo waliteka mapema mwaka 2025. Umoja wa Mataifa, serikali ya Kinshasa na wadau wengine wamekuwa wakilishutumu taifa jirani la Rwanda kwa kulisaidia kundi hilo, madai ambayo Kigali imekuwa ikikanusha.

Ukatili na machafuko mashariki mwa Kongo umeendelea kwa miongo kadhaa, ukisababisha vifo vya maelfu ya watu na kuwafurusha mamilioni kutoka makwao.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *