
Tangu mwezi Januari 2025, pande zote katika mgogoro mashariki mwa DRC zimeshutumiwa kwa kufanya ukiukaji mkubwa wa haki za binadamu na sheria za kimataifa za kibinadamu. Hili ni hitimisho la ripoti ya Umoja wa Mataifa kuhusu hali katika mikoa ya Kivu Kaskazini na Kivu Kusini, iliyochapishwa mwishoni mwa mwaka 2025.
Imechapishwa:
Dakika 2 Wakati wa kusoma
Matangazo ya kibiashara
Ripoti hiyo inataja ukiukaji ambao unaweza kuwa uhalifu wa kivita, au hata uhalifu dhidi ya ubinadamu, na inatoa wito wa kufunguliwa kwa uchunguzi wa jinai. Kwa kukabiliana na shutuma hizi, kila upande unajaribu kutetea msimamo wake. AFC/M23 imetuma ujumbe kwenda Geneva kupinga matokeo ya ripoti hiyo, kando ya kikao cha 61 cha Baraza la Haki za Binadamu, kitachofanyika kuanzia Februari 23 hadi Machi 31, 2026.
Ujumbe wa kutafuta ukweli wa Ofisi ya Kamishna Mkuu wa Haki za Binadamu wa Umoja wa Mataifa ulifanya uchunguzi nchini DRC, Rwanda, na Burundi kati ya mwezi Machi na Agosti 2025.
Katika ripoti yake, ujumbe huo unasema kwamba ufikiaji wa Goma ulikataliwa kwa amri ya AFC/M23. Kwa hivyo, ujumbe huo unadai haukuweza kutembelea maeneo yanayodhibitiwa na kundi hilo lenye silaha.
Kwa upande wake, AFC/M23 inapinga Tume ya Uchunguzi ya sasa. Kundi hilo la waasi linataja sababu mbili.
Maeneo yanayotakiwa kufanyika kwa uchunguzi
Kwanza, wigo wa kijiografia wa uchunguzi: kulingana na AFC/M23, kupunguza uchunguzi katika baadhi ya maeneo, kwa kuitenga Ituri na Maï-Ndombe, ambapo, inadai, uhalifu mkubwa umeshuhudiwa katika maeneo yaliyo chini ya udhibiti wa serikali, unafanya “haki isiyo sawa.” Kundi hilo linabaini kwamba Umoja wa Mataifa “huangazia kilichofanyika upande mmoja tu na kuacha yale yaliyofanyika upande mwingine,” ikimaanisha, kwa maoni ya kundi hilo la waasi, ni sawa na kuficha maovu ya serikali kimakusudi.
Sababu ya pili: mfumo wa muda. AFC/M23 inapinga madai kwamba uchunguzi unaanza mwezi Januari 2025. Kulingana na kundi hilo, chaguo hili linafuta miaka ya maonyo, mateso, na hotuba za chuki zilizoshuhudiwa tangu mwaka 2017 na huchangia “kubuni hoja kwamba mhusika mmoja anawajibika kwa maovu yote yaliyoshuhudiwa DRC.”
Kwa upande wake, ujumbe huo unabainisha uzito wa uhalifu huo na unasema kwamba umekusanya faili zinazowatambua watu binafsi, vitengo na makampuni, yanayoweza kuwajibika kwa ukiukwaji huu na ukiukwaji wa haki za binadamu.
Ujumbe huo unasema faili hizi zimetumwa “kwa mifumo husika ya uwajibikaji.”