Chanzo cha picha, Getty Images
Iliyochapishwa
Muda wa kusoma: Dakika 4
Kauli za hivi karibuni za Rais wa Marekani Donald Trump kuhusu Iran na uwezekano wa kufikiwa kwa makubaliano kupitia mazungumzo kati ya nchi hizo mbili zinapaswa kuchukuliwa kwa uzito, kwa sababu yeye ni rais wa taifa lenye nguvu kubwa zaidi duniani, yaani Marekani.
Katika mkutano wa NATO uliofanyika nchini Uturuki, Donald Trump alitoa kauli kali kuhusu Iran, akisema: “Sitaki tena kuzungumza nao. Ni watu wabaya sana. Je, mnajua watu wabaya ni akina nani? Hao ni watu wabaya. Ni watu wenye fikra potovu. Uongozi wao uko mikononi mwa watu wenye akili iliyopotoka. Ni watu wakatili na wenye kutumia vurugu.”
Aliongeza: “Kama wangekuwa na silaha za nyuklia, wangezitumia. Kwa mtazamo wangu, suala hili sasa limefikia ukomo.”
Lakini je, haya ndiyo maneno ya mwisho ya Trump kuhusu Iran?
Inaonekana huo sio ukweli. Amekuwa akitoa kauli mfululizo kuhusu vita na hati ya makubaliano. Msimamo wake wakati mwingine umejumuisha madai ya ushindi, vitisho vya kuangamiza ustaarabu wa Iran, na hata kuunga mkono mazungumzo.
Baadaye, Trump aliongeza makali ya vitisho vyake vya hivi karibuni, akisema kwamba Marekani “huenda ikawashambulia tena usiku wa jana (Jumatano kuelekea Alhamisi) kwa nguvu zaidi.” Alisema, “Niliwapa onyo kidogo. Tutawashambulia tena usiku wa leo.”
Hii ina maanisha nini?
Chanzo cha picha, NurPhoto via Getty Images
Hakuna shaka kuhusu uwezo wa Marekani wa kuisababishia Iran uharibifu mkubwa.
Hata hivyo, hadi sasa Marekani haijaweza kuilazimisha serikali ya Iran kuachana na madai yake ya msingi, yakiwemo kudhibiti usafiri wa majini katika Mlango wa Bahari wa Hormuz.
Kuhusu serikali ya Iran, Trump alisema, “Hawa wote ni watu wa uongo.”
Kauli hizi zinaweza kutafsiriwa kama kukiri kwamba, licha ya matamshi makali, rais wa Marekani hana chaguo bora zaidi isipokuwa kufanya mazungumzo.
Marekani na Israel zilijaribu kuidhoofisha serikali ya Iran wakati wa mvutano na Iran, lakini juhudi hizo hazikufanikiwa.
Hata hivyo, mazungumzo yako katika hatua muhimu.
Chanzo kimoja kinachohusika katika juhudi za upatanishi kilisema kuwa mazingira ya mazungumzo ni “yenye mvutano mkubwa sana.”
Kwa lugha ya kidiplomasia, hii ina maana kwamba matukio ya siku chache zilizopita yamekuja wakati ambapo mazungumzo yanaendelea kati ya nchi mbili ambazo zina kiwango cha karibu sifuri cha kuaminiana, na hakuna upande unaoamini kwamba mwenzake atatekeleza ahadi zake iwapo makubaliano yatafikiwa.
Serikali ya Iran imeazimia kuendelea kudhibiti Mlango wa Bahari wa Hormuz. Uwezo wa kuzuia njia hiyo inayotumiwa na takriban theluthi moja ya tano ya meli za mafuta na gesi duniani unaipa Iran nguvu ya kushinikiza uchumi wa dunia.
Chaguo hili linachukuliwa kuwa silaha yenye uwezo mkubwa zaidi kuliko uwezekano wa Iran kujaribu kutengeneza silaha ya nyuklia.
Je, Iran itaachia udhibiti wa Mlango wa Bahari wa Hormuz?
Chanzo cha picha, Anadolu/Getty Images
Iran haitakuwa tayari kuachana na udhibiti wake wa Mlango wa Bahari wa Hormuz.
Ndiyo maana iko tayari hata kuhatarisha hati ya Makubaliano, licha ya kwamba makubaliano hayo yanajumuisha masharti kadhaa yanayoweza kunufaisha Iran.
Iran inataka kutuma ujumbe kwamba mambo hayatarejea jinsi yalivyokuwa awali. Inaonekana iko tayari kuhatarisha vita vya muda mrefu ili kulinda kile inachokiona kuwa haki yake katika Mlango wa Bahari wa Hormuz.
Kushindwa kwa juhudi za Marekani na Israel za kuipindua serikali ya Iran kumeongeza ari ya utawala wa Iran. Pia, mazishi ya Kiongozi Mkuu wa Iran yalionyesha kwamba mfumo wa Kiislamu wa kidemokrasia bado unaungwa mkono kwa kiwango kikubwa.
Iwapo mvutano unaoongezeka kati ya pande hizo mbili utaweza kudhibitiwa, wapatanishi wanaoshiriki katika mchakato wa mazungumzo wanaamini kuwa inawezekana kufikiwa kwa makubaliano na Iran ambayo yataruhusu usafiri wa meli kuendelea kupitia Mlango wa Bahari wa Hormuz.
Hili litahitaji makubaliano mapana zaidi ambayo yatarejesha mali za Iran zilizozuiwa nje ya nchi, kuiruhusu Iran kuuza mafuta yake, na, muhimu zaidi, kutambua kwamba Iran itaendelea kuwa na udhibiti wa Mlango wa Bahari wa Hormuz.
Kwa upande wake, Iran italazimika kukubali vikwazo vya urutubishaji wa madini ya urani, kurejesha ufikiaji wa wakaguzi wa nyuklia wa Umoja wa Mataifa, na kutoa maelezo kuhusu akiba ya kile ambacho Rais wa Marekani Donald Trump anakitaja kuwa “vumbi la nyuklia,” akimaanisha urani iliyorutubishwa hadi kufikia kiwango kinachokaribia kutumika kutengeneza silaha ya nyuklia.
Hata hivyo, matukio ya saa 24 zilizopita yameweka wazi jinsi itakavyokuwa vigumu kufikia makubaliano ya aina hiyo.