BODI ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB) imeanza mwaka 2026 kwa kasi ikivuka malengo kwa kukusanya zaidi ya Sh bilioni 60.83 za ukusanyaji wa marejesho ya mikopo kwa miezi mitatu mfululizo. Aidha, malengo ya bodi hiyo yalikuwa kukusanya zaidi ya Sh bilioni 54.99 katika kipindi hicho cha Januari hadi Machi mwaka huu.Mkurugenzi Mtendaji wa HESLB, Dk Bill Kiwia alisema hali hiyo inaashiria kuimarika kwa nidhamu ya urejeshaji na ufanisi wa mifumo ya ukusanyaji.

Akifafanua makusanyo hayo katika kipindi hicho cha miezi mitatu, Dk Kiwia alisema Januari hadi Machi mwaka huu bodi ilipanga kukusanya zaidi ya Sh bilioni 18.33 kila mwezi. Hata hivyo, ilifanikiwa ku vuka malengo na Januari makusanyo yalikuwa zaidi ya Sh bilioni 20.43, sawa na ufanisi wa asilimia 111.SOMA: Kutuma maombi Bodi ya Mikopo mwisho Agosti 31

Ameeleza kuwa makusanyo ya Februari mwaka huu yalifikia zaidi ya Sh bilioni 19.49 ikiwa ni ufanisi wa asilimia 106 na mafanikio makubwa zaidi yalionekana Machi, kwani makusanyo yalipanda hadi kufikia zaidi ya Sh bilioni 20.91 sawa na ufanisi wa asilimia 114. “Hivyo, kwa ujumla katika kipindi hicho tumekusanya marejesho ya zaidi ya Shilingi bilioni 60.83 wakati lengo lilikuwa kukusanya Shilingi bilioni 54.99,” alisema Dk Kiwia.

Amesema mwenendo huo unaonesha kuongezeka kwa makusanyo kadri miezi inavyosonga mbele jambo linaloipa HESLB uwezo mkubwa zaidi wa kugharamia wanafunzi wapya na wanaoendelea na masomo ya elimu ya juu nchini. Akitoa taarifa za wanufaika ambao mikopo yao imeiva na wanapaswa kurejesha ili wengine wanufaike, Dk Kiwia amesema wanufaika 539,103 ambao mikopo yao imeiva wanadaiwa Sh trilioni 2.76.

Hata hivyo, juhudi na mifumo ya ukusanyaji ya HESLB imewezesha kukusanya marejesho ya zaidi ya Sh trilioni 1.84 kutoka kwa wanufaika 403,917 waliotambuliwa na kuanza kurejesha mikopo yao.Amesema pamoja na marejesho hayo, wanufaika 135,186 wanaodaiwa zaidi ya Sh bilioni 920 hawajaanza kulipa, licha ya mikopo yao kuiva. “Bodi inaendelea kuongeza juhudi za kuwatafuta hawa na kuwahimiza kulipa kwa wakati ili kuhakikisha uendelevu wa mpango wa mikopo ya wanafunzi wenye mahitaji na sifa,” alisema.

Amesema mwaka wa fedha 2025/2026 umekuwa wa kuvutia na katika kipindi cha miezi tisa iliyopita pekee bodi hiyo imekusanya zaidi ya Sh bilioni 175.9, sawa na ufanisi wa asilimia 106.6 ya lengo la kukusanya Sh bilioni 165 katika kipindi hicho. Amesema mafanikio haya yanaonesha ongezeko la viwango vya malipo na ufanisi ulioboreshwa katika kufuatilia na kukusanya mikopo kutoka kwa wanufaika. Aidha, Dk Kiwia alisema lengo la bodi la mwaka mzima lilikuwa kukusanya Sh bilioni 220.3 na kwa kuzingatia mwenendo wa sasa wa makusanyo, bodi hiyo inatarajia kukusanya zaidi ya Sh bilioni 225 hadi kufika Juni 30, mwaka huu.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *