Dodoma. Serikali imesaini mkataba wa kukamilisha mpango wa ufadhili wa pamoja wenye thamani ya takribani dola za Marekani 1.277 bilioni (takriban Sh3.34 trilioni) kwa ajili ya kuendeleza mtandao wa Reli ya Kisasa (Standard Gauge -SGR) kipande cha tatu na cha nne kutoka Makutupora ya mkoani Singida hadi Isaka.

Hafla ya utiaji saini wa mkataba huo umefanyika jijini Dodoma na Katibu Mkuu Wizara ya Fedha, Dk Natu El-maamry Mwamba kwa upande wa Serikali na Ofisa Mtendaji Mkuu wa Benki ya Standard Chartered, Herman Kasekende.

‎Akizungumza wakati wa utiaji saini wa mkataba huo, Waziri wa Fedha, Balozi, Khamis Musa Omar amesema fedha hizo ambazo ni sehemu ya jumla ya dola za Marekani bilioni 2.33 za utekelezaji wa mradi huo, ni mpango wa ufadhili wa pamoja kutoka Italia (SACE), Sweden (EKN) na Poland (KUKE), kupitia taasisi zao za dhamana za mikopo ya mauzo ya nje (Export Credit Agencies) za SACE, EKN na KUKE, kwa kuratibiwa na Benki ya Standard Chartered.

 ‎”Uwekezaji huu unaendeleza moja ya miradi ya kimkakati katika historia ya taifa letu, uliolenga kuunganisha Bandari ya Dar es Salaam na Kanda ya Ziwa pamoja na nchi jirani, huku ukiimarisha nafasi ya Tanzania kama kitovu cha biashara na usafirishaji katika ukanda huu,” alisema Balozi Omar.

‎Alieleza kuwa mradi huo si tu uwekezaji mkubwa wa miundombinu, bali ni mradi wa kitaifa wa mfano unaoakisi dira ya muda mrefu ya maendeleo ya Tanzania na ni uwekezaji wa kimkakati wa Taifa, pia ni kichocheo kikuu cha kufanikisha malengo ya muda mrefu ya maendeleo.

Aidha, Balozi Omar alisema kuwa mradi huo ukiendeshwa kikamilifu kwa umeme, ni miongoni mwa njia za usafiri zenye ufanisi mkubwa wa matumizi ya nishati na uzalishaji mdogo wa hewa ukaa, hivyo kuiweka Tanzania mstari wa mbele katika kuelekea uchumi wa kaboni ndogo na unaostahimili mabadiliko ya tabianchi.

Naye Waziri wa Uchukizi, Profesa Makame Mbarawa alisema kuwa Mradi wa SGR utakapokamilika utawawezesha kusafirisha hadi tani milioni 5 za mzigo kwa mwaka na kupunguza kwa kasi kubwa muda wa usafirishaji wa mizigo hali ambayo itaboresha usalama, ufanisi na uendelevu.

‘‘Mradi huu wa kimkakati tayari umeanza kuleta mapinduzi makubwa ya kiuchumi na kijamii, ambapo huduma kati ya Dar es Salaam na Dodoma zimeshasafirisha takriban abiria milioni sita na tani 120,000 za mizigo. Pia umepunguza muda wa kusafiri kutoka saa 12 hadi saa 3 pekee, huku ukichochea utunzaji wa mazingira kwa kupunguza matumizi ya mafuta kwa lita milioni 17 na kupunguza uzalishaji wa hewa ukaa kwa zaidi ya asilimia 50,” alifafanua Mbarawa.

Alisema mkataba uliosainiwa utawawezesha kupanua reli hadi maeneo muhimu na kuiunganisha nchi za jirani kuimarisha biashara, kupunguza gharama za usafirishaji na kufungua fursa za kikanda.

Kwa upande wao mabalozi wa nchi za Sweden, Charlotta Marcias; Balozi wa Italia, Giuseppe Sean Coppola na Mwakilishi wa Balozi wa Poland nchini,  Sergiusz Wolski, kwa nyakati tofauti wameeleza kuridhishwa na uendelezaji wa mradi wa reli ya kisasa (SGR) na kuwa ni kielelezo cha uhusiano imara wa kidiplomasia na kiuchumi kati ya Tanzania na nchi hizo.

Wamesema mafanikio yaliyopatikana katika Loti ya 1 na 2 yamefungua milango ya ushirikiano mpana zaidi katika loti zinazofuata.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *